• Nairobi
  • Last Updated April 16th, 2024 10:55 AM
KILIMO: Wanachopaswa kuzingatia wakulima kupata soko la maparachichi ‘majuu’

KILIMO: Wanachopaswa kuzingatia wakulima kupata soko la maparachichi ‘majuu’

Na SAMMY WAWERU

KWA mujibu wa takwimu za utafiti wa shirika la International Trade Centre (ITC) mwaka wa 2017, Kenya imeorodheshwa kuwa muuzaji mkuu wa maparachichi kutoka Barani Afrika.

Kulingana na ripoti hiyo ya ITC, Kenya huzalisha kadri ya tani 191,000 kila mwaka.

Aidha, huuza karibu tani 51,507 katika soko la kimataifa na kukadiriwa kuingiza mapato ya Sh8bilioni. Afrika Kusini inafuata kwa karibu, ambapo huuza tani 43,492 kwa mwaka.

Kuimarika kwa kilimo cha maparachichi almaarufu avocado nchini, mwaka uliopita kulitia wakulima wengi tabasamu baada ya kiongozi wa nchi Uhuru Kenyatta na Rais wa China Xi Jinping kutia saini mkataba wa makubaliano wa mazao ya Kenya kuuzwa nchini humo.

Hata hivyo, miezi tisa baadaye tabasamu hiyo haipo baada ya mamlaka ya Kilimo na Chakula Nchini, AFA, kusitisha kwa muda usiojulikana uuzaji wa maparachichi katika soko la nje.

Kulingana na AFA, baadhi ya kampuni na mashirika ya wauzaji mazao nje ya nchi na mawakala wanashinikiza wakulima kuvuna matunda ambayo hayajakomaa, suala ambalo linapaka tope sura ya Kenya katika soko la kimataifa.

Wataalamu wa kilimo wanahoji maparachichi yanapovunwa kabla kukomaa, kilele chake bila shaka kitakuwa kuharibika.

“Avocado ambazo hazijakomaa zikivunwa hazitaiva, zinaharibika,” anaonya Daniel Mwenda kutoka Mwenda D Agroforestry Solutions, shirika la kibinafsi linaloangazia masuala ya miti na matunda.

Kwa mujibu wa maelezo ya mdau huyo, kuna vigezo kadha wa kadha ambavyo vinapaswa kuongoza mkulima kujua iwapo maparachichi yamekomaa. Mosi, mengi hubadilisha rangi Mwenda akieleza kwamba kuna yanayogeuka kijani kuwa kijani kibichi (dark green). “Pia kuna aina ya maparachichi yanayogeuka kuwa meusi,” aongeza kueleza.

Mwenda pia anasema njia nyingine kutambua ikiwa matunda hayo yamehitimu kuvunwa, ni kwa kutikisa “ukiskia sauti ya mbegu inayocheza ndani ni ishara kuwa yamekomaa”.

Mtaalamu huyo hata hivyo anasema mkulima asipozingatia vigezo bora vya kilimo, matunda hayo huanza kuanguka kabla kukomaa. Anaiambia Akilimali kuwa kinachosababisha hilo ni mti wa parachichi kukosa madini faafu ambayo ni Boron na Nitrogen.

“Ni muhimu mkulima kabla kuingilia kilimo chochote kile akaguliwe udongo katika maabara ya shughuli hiyo kujua kiwango chake cha rutuba na asidi,” apendekeza, akiongeza kwamba shamba linalopaniwa kukuzwa avocado udongo utolewe hadi kimo cha futi tano na katika sehemu mbalimbali shambani.

Udongo

Anafafanua kuwa, miti ya maparachichi hupenyeza mizizi yake ardhini hivyo basi ni muhimu udongo kukaguliwa kwa kina. “Mimea kama nyanya udongo wake unaweza kutolewa hadi kimo cha futi mbili, mizizi yake si mirefu ikilinganishwa na ya avocado,” Mwenda asema.

Maparachichi yanastawi maeneo yanayopokea mvua ya kutosha, mtaalamu huyo akipendekeza wakulima kukumbatia mfumo wa kunyunyuzia mimea maji kwa mifereji, ndio Irrigation. Udongo tifutifu na usiotuamisha maji ndio bora.

Lucy Ndung’u ni mkulima wa maparachichi Kaunti ya Murang’a na anasema hukuza aina ya Hass ya kupandikiza. Yanathaminiwa kwa kiasi chake kikuu cha uzalishaji, miti inayodumu zaidi ya miaka 50 pamoja na kuwa na mafutahai. “Soko la Hass si kikwazo kamwe kwa mkulima,” Lucy anasema. Akitilia mkazo kauli hiyo, mtaalamu Mwenda anasema soko la aina ya Fuerte pia linaanza kunoga.

Mwenda anasema ikiwa kuna matunda rahisi mno kukuza yakupe mapato, “yaite maparachichi”. Shamba likiwa tayari, andaa mashimo yenye kina cha urefu wa futi mbili na upana wa futi mbili pia. “Kati ya mashimo na laini, isipungue nafasi ya mita tano,” mtaalamu huyo anashauri.

Udongo wa juu uchanganye na mbolea, kipimo cha asilimia 50 kwa 50. Mchanganyiko huo, urejeshe hadi kimo cha asilimia 90 ya shimo, panda mche kisha umwagilie maji. Asilimia 10 iliyosalia ni ya utunzaji, kwa njia ya mbolea, maji na kuweka nyasi za boji ili kuzuia uvukuzi.

Kulingana na Mwenda, muhimu zaidi katika kilimo cha avocado ni usafi; palizi kila makwekwe yanapomea.

“Mbali na maji na usafi wa hadhi ya juu shambani, pogoa matawi usalie na machache ili mazao yawe bora. Matawi mengi huleta ushindani mkali wa maji na mbolea. Mbolea tumia ile hai ya mifugo na fatalaiza kunawirisha mazao,” ashauri.

Magonjwa sugu katika kilimo cha maparachichi ni Damping-off na Bacterial wilt, wadudu wakiwa viwavi, mchwa na panzi.

Chini ya vigezo bora vya kilimo, mazao ya kwanza yanajiri miezi saba baada ya upanzi. Mwenda anasema kiwango cha mazao huongezeka mparachichi unapoendelea kukomaa, akidokeza kwamba mwaka wa pili na nne huzalisha wastani wa matunda 500, mwaka wa nane ukizalisha hata zaidi ya 1,000. Ekari moja inasitiri kati ya miti 80 – 100.

Maparachichi yanayouzwa nje ya nchi, moja hugharimu kati ya Sh15 – 22.

You can share this post!

KILIMOMSETO: Mbegu bora za nyanya zamvunia mamilioni ya hela

SEKTA YA SUKARI: Ripoti ya kufufua sekta ya sukari yatoa...

adminleo