• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 12:58 PM
City yasema heri Sane aozee benchi badala ya kuuzia Bayern kwa bei ya kutupa

City yasema heri Sane aozee benchi badala ya kuuzia Bayern kwa bei ya kutupa

Na CHRIS ADUNGO

MANCHESTER City wamesema itakuwa heri zaidi kwa kiungo Leroy Sane kuingia katika mwaka wa mwisho katika mkataba kati yake nao na awe huru kuondoka bila ada yoyote kuliko kuzinadi huduma zake hadi Bayern Munich kwa bei ya kutupa.

Bayern ambao ni miamba wa soka ya Ujerumani wamekuwa wakivizia huduma za Sane ambaye ni nyota wa zamani wa Schalke 04 nchini Ujerumani, kwa miezi 12 iliyopita.

Kubwa zaidi linachochochea hamasa yao ni ungamo la hivi karibuni la Sane ambaye amesisitiza kwamba hafurahii maisha yake uwanjani Etihad, Uingereza na atakuwa radhi kurejea Ujerumani kuvalia jezi za Bayern ambao kwa sasa wananolewa na kocha Flick Hansi.

Licha ya kutokuwa sehemu ya kikosi cha kwanza cha Man-City katika michuano muhimu, kocha Pep Guardiola amesisitiza kwamba Sane, 24, bado yupo katika mipango ya baadaye ya miamba hao wa soka ya Uingereza.

Ingawa amekiri kwamba Man-City watakuwa tayari kumtia Sane mnadani iwapo mnunuzi ‘mzuri zaidi’ atajitokeza, Guardiola ameshikilia kwamba Sh4.9 bilioni ambazo Bayern wametaka kuweka mezani kwa minajili ya kiungo huyo mvamizi ni “dharau” kubwa.

“Heri asalie nasi, mkataba wake utamatike na ateue pa kuelekea hata bila ya ada yoyote ya usajili. Itakuwa heri zaidi kushuhudia hilo kuliko kumpoteza Sane kwa fedha ambazo kimsingi, zinatosha kujinasia huduma za mwanasoka yeyote wa kawaida au hata wa kiwango cha chini zaidi. Mbona Bayern wanatudharau hivi?” akauliza Guardiola ambaye pia amewahi kudhibiti mikoba ya vikosi vya Barcelona (Uhispania) na Bayern.Kabla ya Sane kupata jeraha baya la goti ambalo limemweka nje kwa kipindi kirefu msimu huu, Man-City walikuwa radhi kumuuza kwa Sh14 bilioni huku Bayern wakijitokeza na Sh9 bilioni mwanzoni mwa muhula huu.

Kwa mujibu wa Guardiola, Sane alikuwa mhimili mkubwa katika mafanikio yao ya msimu wa 2017-18 katika EPL na bei yake kwa sasa, licha ya kusumbuliwa na jeraha, haistahili kushuka chini ya Sh10 bilioni.

Ilivyo, dalili zote zinaashiria kwamba Man-City hawapo tayari kumuuza Sane na watakuwa radhi kumdumisha ugani Etihad kwa msimu mwingine hata kama hatakuwa sehemu muhimu katika kampeni zao za muhula ujao wa 2020-21.

Hadi kusitishwa kwa shughuli zote za soka ya Uingereza kutokana na janga la corona mnamo Machi 2020, Sane hakuwa amewajibishwa katika mchuano wowote tangu apate jeraha katika gozi la Community Shield baina yao na Liverpool mnamo Agosti 2019.

Alirejelea mazoezi mepesi mwanzoni mwa Februari 2020 na mchuano wake wa kwanza ulitazamiwa kuwa dhidi ya Watford mnamo Mei 9 ugani Vicarage Road, Uingereza.

You can share this post!

Serikali Ujerumani yaruhusu kipute cha Bundesliga...

Usimamizi wa Tusker sasa unakarabati uwanja wao wa Ruaraka

adminleo