• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 1:29 PM
Mwanaraga wa zamani ateuliwa kocha wa Kenya Rugby League

Mwanaraga wa zamani ateuliwa kocha wa Kenya Rugby League

Na CHRIS ADUNGO

MWANARAGA nguli Edward Rombo ameteuliwa kuwa kocha wa timu ya taifa ya Kenya Rugby League.

Rombo ataongoza programu ya timu ya taifa na kushirikiana na wakfu wa Giving Rugby Foundation kupiga jeki juhudi za benchi ya kiufundi na Shirikisho la Raga la Kenya katika makuzi ya vipaji miongoni mwa wanaraga wa humu nchini.

Nyota huyo wa zamani wa timu ya taifa ya Kenya, anajivunia tajriba ya takriban miaka 30 ya uchezaji na ukufunzi katika Ligi na Shirikisho la Raga. Ndiye Mkenya wa kwanza kuwahi kusakatia kikosi cha Leeds Rugby, Dewsbury na Featherstone Rovers, Uingereza katika miaka ya 90.

Rombo ambaye ni fowadi, anajivunia misimu mingi ya kuridhisha katika Raga ya Shirikisho hasa ikizingatiwa kwamba aliwahi kuwaongoza Mean Machine kujizolea ubingwa wa Ligi Kuu ya Kenya Cup mnamo 1989 na 1990. Amewahi pia kuchezea klabu za Watembezi Pacesetters na Barclays RFC.

Rombo, anayemiliki kampuni ya masuala ya uanasheria ya Rombo and Co Advocates, amewahi pia kuwa kocha wa kikosi cha Mwamba RFC.

“Nikiwa mwasisi wa Rugby League nchini Kenya, itakuwa fahari yangu kuona mchezo huo ukikita mizizi na kuwa kivutio cha wanaraga wa haiba watakaojitolea kuunda kikosi thabiti kitakachovaana vilivyo na vigogo wengine duniani,” akasema Rombo.

Nyakwaka Adhere ambaye ni mwenyekiti wa Kenya Rugby League amesema kwamba shughuli za kuteua timu ya taifa na mazoezi ya wanaraga hao kwa sasa imeahirishwa kutokana na janga la corona.

Aliongeza kwamba pindi corona itakapodhibitiwa, maskauti wataanza kuteua wachezaji watakaounga timunya taifa kwa minajili ya mchuano utakaokutanisha Kenya na Afrika Kusini katika uwanja na tarehe itakayofichuliwa baadaye. Tofauti na Raga ya Shirikisho, Rugby League hutandazwa na jumla ya wachezaji 13.

Kipute hicho kiliasisiwa nchini Uingereza na pia kinasakatwa Australia na New Zealand.

Hapa Kenya, mechi za Rugby League huchezewa katika uwanja wa Railways Club, Nairobi.

You can share this post!

Seneta Ledama ole Kina aitwa mahakamani ajibu shtaka la...

BI TAIFA APRILI 1, 2020

adminleo