• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 8:55 AM
Msiingize siasa katika timu zenu za taifa za raga, kocha Ben Ryan ashauri Kenya

Msiingize siasa katika timu zenu za taifa za raga, kocha Ben Ryan ashauri Kenya

Na GEOFFREY ANENE

WANARAGA wa Kenya walinufaika na mafunzo kutoka kwa kocha mtajika Benjamin Ryan kuhusu mbinu inazostahili kutumia kupata matokeo mazuri zikiwemo kutoingiza siasa kikosini, kuwa na maadili mema, kujiamini, kuwa na mtazamo bora na tabia inayokubalika na timu.

Kocha huyo Mwingereza, ambaye aliongoza timu ya wanaume ya Fiji kutwaa medali ya raga ya wachezaji saba kila upande kwenye Olimpiki 2016, alisema pia ni muhimu wachezaji wafanye wanachoweza kwa kuweka mipango kabambe, kujitolea pamoja na kudumisha uhusiano mwema na wachezaji wazoefu na makocha ili waweze kuendelea kupata matokeo mazuri.

“Umoja na uelewano kikosini ni vitu muhimu sana katika utafutaji wa matokeo mazuri katika viwango vya juu,” alisema mshindi huyo wa taji la Raga ya Dunia ya msimu 2014-2015 alilopata pia na Fiji.

Kama kocha, Ryan anasema, ana uhusiano mzuri na viongozi na anatumia mfumo rahisi kuhusu kinachostahili kufanywa. “Tunaweka viwango rahisi, kila mtu anafahamu kinachoendelea, hakuna siasa katika kundi letu la wachezaji ama benchi ya kiufundi,” anasema.

“Elewa wachezaji wako, fahamu kinachowachochea, kinachowapa motisha, punguza wasiwasi wao na mara kwa mara wapatie majibu wanapostahili kuimarika na kumbuka kuwapongeza wanapofanya vyema. Hakikisha unazungumza nao kila mara ili wajisikie salama,” Ryan alishauri katika warsha hiyo iliyofanyika Ijumaa usiku kupitia kwa mtandao.

You can share this post!

Ronaldo afunga penalti na kusaidia Juventus kunyoa Lecce...

Wahubiri wapokea msaada wa chakula kutoka kwa mbunge

adminleo