• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
CHOCHEO: Mfadhaiko wa corona wafanya miereka ya kitandani kupungua

CHOCHEO: Mfadhaiko wa corona wafanya miereka ya kitandani kupungua

Na BENSON MATHEKA

SIO siri kwamba janga la corona limeathiri pakubwa maisha ya mapenzi ya watu wengi. Marufuku ya kusafiri imenyima watu fursa ya kukutana na wapenzi wao.

Watu hawawezi kuzuru maeneo ya burudani kujivinjari na wachumba wao na hata kama maeneo hayo yangekuwa yamefunguliwa, mapato ya watu wengi yamepungua.

Wataalamu wa masuala ya mapenzi wanasema kwamba janga la corona limefanya watu wengi kukosa uwezo wa kutekeleza tendo la ndoa.

“Athari za janga la corona zimefanya watu wengi kukosa hamu ya kula uroda na hii inatishia ndoa nyingi kote ulimwenguni,” mwanasaikolojia Shannon Chavez, aliambia jarida la mtandaoni la Huffpost.

Mwanasaikolojia huyo anasema kwamba hali hii inachangiwa na shinikizo ambazo watu wanapitia kwa kupoteza kazi na mapato yao.

“Ni kawaida ya watu kukosa hamu ya kutekeleza tendo la ndoa wakiwa na mfadhaiko au wanapokabiliwa na masononeko au machungu maishani na athari za janga la corona zimewafanya wengi kukosa matumaini. Katika hali hii watu hukosa uwezo wa kutekeleza tendo la ndoa,” asema Chavez.

Wataalamu wanasema kwamba watu wengi wanafikiria jinsi ya kufufua uwezo wao wa kifedha.

“Janga la corona lilisukuma watu pabaya wakawa na mfadhaiko, wanakosa usingizi na hawana hamu ya kula uroda. Mtu akiwa na mfadhaiko uwezo wa kusakata ngoma chumbani huwa unapungua,” asema Daisy Kawira wa shirika la Maisha Mema jijini Nairobi.

Kulingana na Kawira, kukaa nyumbani kwa wanandoa kwa muda mrefu kunachangia kudorora kwa hamu ya kuburudishana chumbani.

“Wachumba wakikaa pamoja nyumbani, huwa wanaweza kukasirikiana, kuchokana na kukosa kuchangamkiana chumbani. Hali ikiwa hii, hamu ya tendo la ndoa hufifia,” asema Kawira.

Anakubaliana na Chavez kwamba corona imedidimiza hamu na uwezo wa tendo la ndoa wa wachumba wanaoishi pamoja.

Hata hivyo, mwanasaikolojia Christine Koli anasema kukaa nyumbani kunafaa kufanya wachumba kujipanga vyema.

“Muda mwingi wa kuwa pamoja wakati huu wa corona umefanya wanandoa kujipanga upya zaidi kuhusu tendo la ndoa. Wana muda wa kudekezana zaidi hata bila kujamiiana; jambo ambalo ni muhimu katika uhusiano wa kimapenzi,” asema Koli.

Wanasaikolojia wanasema kwamba baadhi ya watu wanakosa hamu na uwezo wa kula uroda kwa sababu ya kutazama picha na video za mapenzi mitandaoni.

“Katika uhusiano wa mapenzi, mchumba mmoja akizama katika ponografia uwezo wake wa tendo la ndoa hupungua na hali huwa mbaya,” aeleza Chavez.

Kulingana na Huffpost, idadi ya watu wanaotembelea mitandao ya ponografia iliongezeka wakati nchi nyingi zilipotangaza watu kukaa nyumbani kuzuia kusambaa kwa virusi vya corona.

Tabia hii imefanya watu wengi kuanza kujichua, kitendo kinachofanya mtu kukosa hamu ya kushiriki tendo la ndoa na mke au mpenzi wake au hata kukosa uwezo wa kufanya mapenzi kabisa.

Koli anasema athari za corona zimesababishia watu matatizo ya kiakili na kuwafanya kutopatia tendo la ndoa kipaumbele katika maisha yao.

“Watu wamesongwa na mawazo. Hawajui kesho itakuwaje. Mawazo waliyo nayo ni jinsi wanaweza kujikwamua kutoka hali ya sasa. Kwao, shughuli za chumbani zinaweza kusubiri,” asema.

Kwa wachumba wanaokaa pamoja, aeleza, hii haifai kuponza uhusiano wao kuliko waliofungiwa maeneo tofauti. Hofu ya wanasaikolojia ni kwamba huenda wanaojichua wakawa watumwa wa tabia hii na kupoteza kabisa uwezo wa kuburudisha wachumba wao.

“Hii ni kwa wanaume na wanawake. Cha muhimu ni kuepuka kutazama ponografia inayovuta watu kuanza tabia hii,” asema Koli.

You can share this post!

FATAKI: Ni unafiki kukejeli wanawake waliokataa kutumia...

UMBEA: Unavyoweza kukabili huzuni ya kuondokewa na umpendaye

adminleo