• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 6:50 AM
WANDERI: Usiishi katika ndoa isiyo furaha ukihofia jamii, dini

WANDERI: Usiishi katika ndoa isiyo furaha ukihofia jamii, dini

Na WANDERI KAMAU

MOJAWAPO ya hatua kuu katika maisha ya mwanadamu hapa duniani ni ndoa. Ndoa huchukuliwa kuwa hatua muhimu sana kuliko zingine, ambazo ni kuzaliwa, tohara na kifo.

Ndoa huwa na uzito mkubwa kwani huathiri mustakabali wa mwanadamu katika muda wa maisha yake atakayohudumu kama mzazi.

Katika mila za Kiafrika, ndoa ndiyo chemichemi na mwanzo wa ukoo, ambao baadaye hukua na kuwa jamii kubwa iendelezayo uzao wa kizazi husika.

Hivyo, tangu enzi za mababu zetu, ndoa ni taasisi muhimu sana katika jamii za Kiafrika hadi sasa.

Lakini licha ya umuhimu wake mkubwa, taasisi hiyo inaonekana kuingia doa, hasa katika kizazi cha sasa.

Kinyume na ilivyokuwa awali, wanandoa wengi wanashambuliana wao kwa wao, baadhi hata wakiuana kutokana na sababu za mizozo ya kifamilia.

Athari za vitendo hivyo vya kusikitisha ni kuwa vinakatiza ndoto na malengo ya kimaisha ambayo wengi hulenga kuyatimiza.

Bila shaka, matukio hayo ya kuogofya ndiyo yamezua maswali na mdahalo mkali wa ikiwa ni kweli lazima mtu aoe au aolewe ndipo aonekane kuwa “mkamilifu” kwa mantiki ya taratibu ambazo zimewekwa na jamii.

Maswali yanayoibuka ni: Je, ndoa ina umuhimu wowote katika maisha ya sasa? Je, jamii itamkumbatia atakayekiuka kanuni zilizowekwa kuhusu ndoa? Lengo la awali la taasisi ya ndoa limebadilishwa na maisha ya kisasa?

Kulingana na mwanafalsafa Aristotle, lengo kuu la mwanadamu kuishi hapa duniani ni kupata furaha.

Hili ni katika kazi ama shughuli zozote za kimaisha azifanyazo—iwe ni kwenye usomi, uanabiashara, uanahabari, ualimu kati ya mengine.

Lengo kuu ni kupata furaha maishani, ambapo uwepo wa ndoa si jambo la lazima.

Vile vile, lengo lingine kuu ni kuhakikisha kuwa mwanadamu, kama sehemu ya uumba wa Mungu, ametimiza wajibu aliokusudiwa hapa duniani.

Mwanafalsafa Voltaire naye anasema kuwa mkasa mkuu katika maisha ya mwanadamu ni kufariki akiwa hajatimiza yale aliyokusudiwa kuyafanya hapa duniani.

Kwenye maisha yake, Voltaire, aliyeishi Ufaransa, aliamini kuwa ingawa ndoa ni mojawapo ya maagizo makuu aliyopewa mwanadamu na Mungu kuyatimiza ili kuongeza uzao wake duniani, si lazima ijumuishwe kama mojawapo ya mambo makuu anayopaswa kuyazingatia.

Voltaire anashikilia kuwa lengo kuu la mwanadamu linapaswa kuhakikisha kuwa ametumia vipaji alivyopewa na Mungu kama uimbaji, uandishi, usomi, uchezaji kati ya vingine kuhakikisha kuwa wenzake wamefaidika.

Bila shaka, hizi ni baadhi tu ya nadharia kinzani ambazo zimekuwepo kuhusu fasiri kamili ya “ukamilifu” wa maisha ya mwanadamu.

Kinaya ni kuwa, misimamo kama hii inatofautiana vikali na mafundisho ya kidini, yanayosisitiza kuwa lazima mume aoe mke ili kuendeleza uumba wa Mungu.

Haya ni muhimu, lakini lazima tusikubali kutesekea mikononi mwa mtu kwa kisingizio cha “kuheshimu” kanuni za kijamii ama kidini. Haifai hata kidogo kuishi kwa majonzi maisha yako yote eti kwa sababu haya ni mapenzi ya Mungu. La hasha! Ishi maisha ambayo yatakupa furaha.

[email protected]

You can share this post!

WANGARI: Corona imechangia katika ukuaji wa biashara...

AFYA: Kitendawili kuhusu usahihi wa vipimo, ingawa sio...

adminleo