• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 4:31 PM
Barcelona kupiga kura kumng’oa Bartomeu

Barcelona kupiga kura kumng’oa Bartomeu

Na MASHIRIKA

RAIS wa klabu ya Barcelona, Josep Maria Bartomeu anatazamiwa kuondoka mamlakani baada ya kampeni ya kupigwa kwa kura ya kutokuwa na imani naye kupata uungwaji mkono miongoni mwa wadau wa kikosi hicho cha Ligi Kuu ya Uhispania (La Liga).

Bartomeu alichaguliwa kuwa Rais wa Barcelona mnamo 2014 na uongozi wake umekashifiwa pakubwa kiasi cha kuhusishwa na maamuzi ya hivi karibuni ya nyota Lionel Messi kutaka kuondoka ugani Camp Nou.

Mpango wa kuondolewa kwa Bartomeu kupitia kura ya maoni ulifichuliwa na vinara wa Barcelona siku moja baada ya Messi kuwasilisha barua ya kutaka kuachiliwa kuondoka Camp Nou.

Kufikia sasa, saini 20,731 kutoka kwa mashabiki na wasimamizi wa Barcelona wanaounga mkono mpango huo zimepatikana, kumaanisha kwamba Bartomeu yuko pua na mdomo kuondolewa mamlakani kupitia kura ya wadau kutokuwa na imani naye.

Ili kufanikisha maandalizi ya kura hiyo, jumla ya saini 16,500 pekee ndizo zilizohitajika kuwasilishwa na kukaguliwa na wahusika kabla ya Bartomeu, 57, kuondolewa kupitia refarenda chini ya kipindi cha miezi mitatu ijayo.

Refarenda ya kumng’atua Bartomeu itashuhudia wanachama 150,000 wa Barcelona wakipiga kura na iwapo asilimia 66.5 ya wanachama watapiga kura ya kumwondoa, basi uongozi wake utafikia kikomo.

Bartomeu alitarajiwa kukamilisha rasmi kipindi chake cha uongozi cha mihula miwili mnamo Machi 2021.

Iwapo kura ya kutokuwa na imani naye itaandaliwa, basi atakuwa rais wa tatu wa Barcelona kuondolewa mamlakani kwa jaribio la njia hiyo baada ya Josep Lluis Nunez mnamo 1998 na Joan Laporta mnamo 2008. Mpango wa kung’atuliwa kwa wawili hao kupitia refarenda miaka hiyo haukufaulu.

Messi aliyekuwa akiwaniwa pakubwa na Manchester City ya Uingereza, alihiaria kusalia Barcelona japo huenda akabanduka rasmi baada ya mkataba wake kutamatika mwishoni mwa 2020-21.

Chini ya urais wa Bartomeu, Barcelona wamekabiliwa na visa vya matumizi mabaya ya fedha na kikosi hicho kilikamilisha kampeni za msimu huu bila kutwaa taji lolote kwa mara ya kwanza tangu 2008.

Walibanduliwa mapema na Athletic Bilbao kwenye Copa del Rey, wakapigwa kumbo na Real Madrid kwenye La Liga na kudhalilishwa na Bayern Munich kwa kichapo cha 8-2 kwenye robo-fainali za Klabu Bingwa Ulaya (UEFA).

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Tusiyenge asajiliwa na APR ya Rwanda

Setien kuishtaki Barca