• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 3:25 PM
KRU kuandaa mchujo kwa ajili ya vikosi vya raga kupanda na kushuka ngazi katika ligi za chini

KRU kuandaa mchujo kwa ajili ya vikosi vya raga kupanda na kushuka ngazi katika ligi za chini

Na CHRIS ADUNGO

SHIRIKISHO la Raga la Kenya (KRU) limethibitisha kwamba kutaandaliwa mchujo wa ligi za madaraja ya chini ya Championship na Nationwide ili kuamua vikosi vitakavyopanda na kushuka ngazi kwa minajili ya msimu mpya wa 2020-21.

Boadi ya KRU pia imethibitisha kuwa hapatakuwepo mshindi wa Ligi Kuu ya Kenya Cup wala ligi zote nyinginezo za chini katika msimu wa 2019-20 uliotamatishwa ghafla kutokana na ugonjwa wa Covid-19.

Hali ya Kisumu RFC na Western Bulls, waliokuwa wameshushwa ngazi kwenye Kenya Cup; pamoja na Kisii RFC na Mombasa RFC waliokuwa wameteremshwa ngazi kwenye Championship itasalia vivyo hivyo kwa sababu kampeni zao zilikuwa zimetamatika kabla ya ujio wa corona.

“Kwa mujibu wa sheria za KRU, haitawezekana kwa mshindi wa ligi yoyote kupatikana bila ya mechi za mchujo kuandaliwa. Hivyo, matokeo yaliyokuwa yamesajiliwa hadi wakati wa kutamatishwa kwa kampeni za 2019-20 yatasalia jinsi yalivyo,” akasema Katibu wa KRU, Ian Mugambi.

“Hata hivyo, vikosi vilivyokuwa vimeteremshwa ngazi vitasalia kushuka daraja kwa kuwa mechi zao zilikuwa zimekamilika. Mchujo sasa utaandaliwa ili kuamua timu zitakazopanda na kushuka ngazi kwenye Championship na Nationwide,” akaongeza kinara huyo.

Kwa mujibu wa KRU, muhula wa uhamisho wa wanaraga kwa minajili ya msimu ujao utafunguliwa rasmi kuanzia Oktoba 7 hadi Novemba 30. Hata hivyo, ni wanaraga waliokuwa sehemu ya vikosi vyao katika kampeni za 2019-20 ndio wataruhusiwa kushiriki mchujo.

Vikosi vya raga ya Ligi Kuu ya Kenya Cup vimetaka waliokuwa washiriki wote wa kivumbi cha msimu uliofutiliwa mbali wa 2019-20 kusalia vivyo hivyo katika muhula ujao wa 2020-21.

“Tumependekeza kwamba vikosi vilivyonogesha kampeni za msimu jana visalie jinsi vilivyokuwa kwa minajili ya muhula mpya ujao,” akasema Xavier Makuba ambaye ni mwenyekiti wa vikosi vya Kenya Cup.

Hatua hiyo ni pigo kwa Mean Machine, Chuo Kikuu cha Masinde Muliro, Chuo Kikuu cha USIU, Northern Suburbs na Strathmore Leos ambao hadi kufutiliwa mbali kwa msimu huu, walikuwa wamefuzu kwa mchujo wa Championship wakilenga kujaza nafasi mbili katika Ligi ya Kuu ya Kenya Cup.

Kwa mujibu wa Makuba, vikosi vitakavyosalia kwenye Kenya Cup katika msimu mpya wa 2020-21 ni Kabras, Homeboyz, Impala Saracens, Mwamba, Menengai Oilers, Nakuru RFC, Nondies, Kenya Harlequins, Blak Blad na mabingwa wa 2018-19, KCB.

Japo Makuba amependekeza msimu mpya wa raga uanze Novemba, mkufunzi Mitch Ocholla wa Impala Saracens, ametaka msimu wa 2020-21 uanze Januari mwaka ujao.

“Zipo taratibu nyingine zinazohitaji kutimizwa ili Wizara ya Afya ikubalie michezo kurejelewa. Mojawapo ni kufanyia wanaraga, marefa na maafisa wote wa benchi za kiufundi wa kila klabu vipimo vya corona.”

“Hili ni zoezi ghali mno kutekeleza. Vyema tusubiri zaidi makali ya corona yapungue kabisa ndipo raga irejee kwa vishindo,” akasema Ocholla aliyewahi pia kunoa timu ya taifa ya Shujaa mnamo 2011-12.

You can share this post!

Milioni 1.5 wameambukizwa corona Afrika – kituo...

Wanafunzi wa Kidato cha Nne, Darasa la Nane na Darasa la...