• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
NGILA: Blockchain kwa lugha ya Kiswahili! Heko TZ

NGILA: Blockchain kwa lugha ya Kiswahili! Heko TZ

Na FAUSTINE NGILA

JE, mbali na kung’amua kuwa nchi jirani ya Tanzania inatawaliwa na Rais John Magufuli, ni lipi lingine unalotambua kuhusu nchi hiyo?

Naam, katika ulingo wa teknolojia, Tanzania ni mojawapo ya mataifa yanayopiga hatua kubwa katika kupigia debe uvumbuzi wa kisasa.

Taifa hilo la zaidi ya watu milioni 56 limekuwa katika mstari wa mbele katika kupunguza ada ya matumizi ya intaneti Afrika. Ndilo taifa linaloongoza hapa Afrika Mashariki kwa mauzo ya intaneti ya bei nafuu kwa wananchi.

Tofauti na Kenya ambapo bei ya intaneti ni Sh112 kwa kila GB moja ya data, Tanzania watakulipisha Sh78 pekee kwa wastani, kulingana na utafiti.

Na sasa wiki iliyopita, nchi hiyo imeandika au kufasiri kitabu cha kwanza kabisa kinachoelezea teknolojia ya kisasa ya Blockchain na manufaa yake.

‘Jielimishe Kuhusu Blockchain’ ni kitabu kilichozinduliwa kwa wasomaji mnamo Novemba 20 kupitia mtandao wa kuuza bidhaa mtandaoni nchini Tanzania wa Posta Shop, kinanuia kuelezea kuhusu teknolojia hiyo kwa lugha rahisi kwa Waafrika.

Mwandishi wake, Sandra Chogo, ambaye ni mhadhiri wa masuala ya teknolojia ibuka (4IR) ameiletea Tanzania fahari tele katika ulimwengu wa teknolojia, ikizingatiwa Kiswahili huzungumzwa katika mataifa 15 barani Afrika, huku pia kikiwa na wafuasi nchini Amerika, Ujerumani, Ufaransa, Australia na mataifa ya Uarabuni.

Ingawa Kenya ilikuwa nchi ya kwanza Afrika kuandika kitabu kuhusu Blockchain, ilifanya hivyo kwa lugha ya Kiingereza ambayo wananchi wa mashinani hawawezi kuielewa kwa urahisi.

Ilichofanya Kenya ni majaribio ya kuunda mfumo wa lugha ya kuunda programu za kompyuta na kuchanganua data almaarufu Python kwa kutumia Kiswahili.

Lakini ikalemewa kuandika kitabu cha Kiswahili cha kuelezea wanafunzi kuhusu teknolojia hiyo.

Nimekuwa kwenye safu hii kwa miaka kadhaa sasa, na ninaweza kusema kwa imani kuwa matumizi ya blockchain ni mengi mno, na yana uwezo mkubwa zaidi ya teknolojia zote kutatua matatizo tunayoshuhudua hapa barani.

Kwa mfano, ufisadi, wizi wa kura, uuzaji wa bidhaa ghushi, wizi wa mitandaoni, leseni na vyeti feki na hila zozote zile ni visiki ambavyo vinaweza kuondolewa kwa suluhu za blockchain.

Kwa kuandika kitabu hicho kwa lugha ya Kiswahili, wananchi katika mataifa ya Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi na Sudan Kusini wataweza kuona manufaa ya teknolojia katika kusuluhisha vizingiti katika maisha yao.

Changamoto kuu katika teknolojia za kisasa imekuwa jinsi zinavyoelezwa kwa Waafrika.

Waandishi wengi ni wa mabara ya Ulaya, Amerika na Asia na wamekuwa wakitumia lugha yenye maneno mazito ya Kiingereza yanayoeleweka kwa wasomaji wao.

Lakini sasa Afrika imeanza safari ya kuelezea kuhusu teknolojia nyingine kama Uchanganuzi wa Data, 5G, Uchapisho wa 3D, Teknolojia za Kiotomatiki (AI) ambazo zitapata matumizi yake hapa barani kwa upana.

You can share this post!

Ruto amhepa Uhuru tena

BBI: Uhuru, Raila wapuuza vilio