• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 4:10 PM
AWINO: Nani atawanusuru Wakenya dhidi ‘viriba’ vya wabunge?

AWINO: Nani atawanusuru Wakenya dhidi ‘viriba’ vya wabunge?

Na AG AWINO

WASWAHILI husema kujaliwa leo kesho kuna Mungu.

Yaani wewe binadamu, jishughulishe tu na ya leo, ye kesho ni Mungu tu anayejua.

Waswahili hawakunena haya kwa sababu hivi ndivyo binadamu anavyostahili kuishi, ila walitaka kuangazia hatari iliyopo iwapo hujiangalii wala kujiandaa kwa maisha ya kesho ipasavyo.

Mwishoni mwa wiki, ripoti iliibuka kwamba Wabunge sasa wanataka bidhaa zote ambazo zimekubaliwa kuingia humu nchini kutoka nje zipigwe msasa ili kubaini viwango vya kemikali zilizopo kwenye bidhaa hizo.

Bunge la Kifaifa liliagiza Kamati ya Bunge inayoshughulikia Kilimo, Bodi ya Dawa za Wadudu (PCPB) na Halmashauri ya Ubora wa Bidhaa Nchini (KEBS) kuchunguza upya kiwango cha kemikali kinachopatikana kwenye dawa za kuzuia wadudu na pembejeo.

Wanataka ripoti hii kuletwa chini ya siku 90. Lengo lao likiwa hasa kutambua bidhaa zisizohitajika katika soko la humu nchini kutokana na hatari zinazosababishwa nazo.

Habari kuhusu kemikali zinazohatarisha maisha ya Wakenya zimekuwako tangu jadi.

Mwaka 2019, ripoti ya Shirika moja la Kigeni likishirikiana na Hospitali kuu Moi ilionyesha kwamba wanawake wengi walio katika maeneo ya ukuzaji mahindi – Trans-Nzoia na Bungoma- walikuwa wakiugua saratani ya Uzazi.

Mojawapo ya sababu iliyotolewa ni kwamba mahindi waliyoyala yana kiwango cha juu cha kemikali aina ya aflatoxin ambayo imehusishwa sana na kansa ya uzazi.

Mashirika mbalimbali, aidha yamejaribu kurai wananchi dhidi ya matumizi ya kemikali za kuzuia magugu na hata pembejeo kwani zina kiwango kikubwa cha kemikali hatari.

Madai haya sasa yamethibitishwa baada ya vuta nikuvute baina ya wafanyibiashara wenye njeje nzito na wabunge kubaini kuwa wamekuwa wakichezea maisha ya Wakenya kwa sababu ya pupa wa faida.

Ripoti kwamba baada ya KEBS kutahadharisha kwamba kampuni nyingi za kimataifa zilikuwa zikileta pembejeo za viwango vya chini na zilizokuwa na kemikali hatari aina ya Cadmium, wabunge waliwekewa shinikizo na wafanyibiashara hawa mnamo 2018.

Shinikizo zilikuwa nzito sana hivi kwamba walilazimika kupiga kura kuwakubalia kuendelea kuleta pembejeo hatari yenye bei nafuu nchini.

Ingawa kiwango cha kemikali ni asilimia 15 tu, walishinikizwa kukubali pembejeo yenye asilimia 60 ya kemikali.

Nyongeza ya asilimia 45.

Kwa kuwa pembejeo na dawa za kuzuia wadudu zenye viwango vya chini vya kemikali ni ghali, waagizaji wanapenda bidhaa zenye viwango vya juu kutokana na faida kubwa wanazopata.

Wakenye wajue hawana wa kuwajali. Tangu lini ukweli wa kisayansi ukawekwa katika kura ya maamuzi? Iwapo wanasayansi wameshashema kwamba kuna hatari fulani, sharti wasikilizwe.

Hata hivyo, kutokana na ‘bahasha’ nono, kwa miaka mitatu, Wakenya wamekuwa wakitumia pembejeo ambazo zinahatarisha maisha yao.

Bado tunajiuliza ni kwa nini tuna visa vingi vya watu wanaougua saratani na wengi wao kuaga dunia?

Kwa maoni yangu, agizo hilo la Bunge ni drama na sinema ambayo kila mara huwekwa wakati bahasha ‘hazijatembea’. Aidha, ni juhudi kiduchu baada ya muda mwingi kupita. Ni sawa na kilio cha chura kisichomzuia ng’ombe kunywa maji.

Kisa hiki kinanikumbusha madhara ya bomu la kiatomiki ambalo liliangushwa Hiroshima na Nagasaki, Japan mnamo 1945. Hadi wa leo, miaka 75 baadaye, madhara ya bomu hili bado yanashuhudiwa nchini humo.

Ni nani atakayewasaidia Wakenya dhidi ya viriba vya Wabunge na waagizaji ambao wamejitajirisha sana huku mamilioni wakisafirishwa ahera?

Bw Awino ni mwanamawasiliano anayeandika kuhusu masuala ya kilimo,

[email protected]

You can share this post!

Corona yasukuma milioni 2 kwa dhiki

Ruto amhepa Uhuru tena