• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 11:14 AM
Wanasoka wanne wa Liverpool kuwania tuzo ya FIFA ya Mchezaji Bora wa Mwaka 2020

Wanasoka wanne wa Liverpool kuwania tuzo ya FIFA ya Mchezaji Bora wa Mwaka 2020

Na MASHIRIKA

WANASOKA Virgil van Dijk, Mohamed Salah, Sadio Mane na Thiago Alcantara wa Liverpool wameteuliwa kuwania taji la Mwanasoka Bora wa Mwaka 2020 katika tuzo za Best Fifa Football zitakazotolewa na Shirikisho la Soka Duniani (FIFA) mnamo Disemba 17, 2020.

Kiungo wa Manchester City, Kevin de Bruyne pia yuko katika orodha ya wachezaji 11 ambao wameteuliwa kuwania ubingwa wa taji hilo kwa upande wa wanaume.

Beki Lucy Bronze wa Man-City na timu ya soka ya wanawake nchini Uingereza pia amejumuishwa katika orodha ya wachezaji 11 wa kike watakaopigania tuzo hiyo.

Jurgen Klopp wa Liverpool na Marcelo Bielsa wa Leeds United wanakamilisha orodha ya wakufunzi watano watakaowania taji la Kocha Bora wa Mwaka. Orodha hiyo inajumuisha pia Hans-Dieter Flick (Bayern Munich ya Ujerumani), Julen Lopetegui (Sevilla ya Uhispania) na Zinedine Zidane (Real Madrid ya Uhispania).

Kocha Emma Hayes wa kikosi cha wanasoka wa kike kambini mwa Chelsea atatoana jasho na kocha Sarina Wiegman wa timu ya taifa ya Uholanzi. Wiegman anatazamiwa kutwaa mikoba ya timu ya soka ya wanawake nchini Uingereza kuanzia Septemba 2021.

Kwa mujibu wa FIFA, walioteuliwa kuwania tuzo hizo watapigiwa kura na wawakilishi 200 wa vyombo vya habari na makocha wote wa timu za taifa kote duniani kupitia mtandaoni.

Shughuli ya kupiga kura itaanza rasmi mnamo Novemba 25, 2020 na kukamilisja Disemba 9, 2020.

Bao lililofungwa na fowadi wa Tottenham Hotspur, Son Heung-min dhidi ya Burnley katika mechi ya Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) mnamo Oktoba 26, 2020 limeteuliwa kuwania tuzo ya Goli Bora zaidi la mwaka almaarufu ‘Puskas Award’.

Goli lililofungwa na nahodha wa timu ya taifa ya soka ya wanawake nchini Wales, Sophie Ingle akichezea Chelsea dhidi ya Arsenal katika Women’s Super League limeteuliwa pia kuwania taji la Puskas Award. Bao lake litashindana na lile lilifumwawavuni na fowadi wa Scotland, Caroline Weir alipokuwa akichezea Man-City dhidi ya Manchester United. Bao jingine linalopigania tuzo hiyo ni ni lile lilifumwa wavuni na Jordan Flores wa Dundalk dhidi ya Shamrock Rovers.

MCHEZAJI BORA – WANAUME:

Thiago Alcantara (Uhispania, Liverpool)

Cristiano Ronaldo (Ureno, Juventus)

Kevin de Bruyne (Ubelgiji, Manchester City)

Robert Lewandowski (Poland, Bayern Munich)

Sadio Mane (Senegal, Liverpool)

Kylian Mbappe (Ufaransa, Paris St-Germain)

Lionel Messi (Argentina, Barcelona)

Neymar (Brazil, Paris St-Germain)

Sergio Ramos (Uhispania, Real Madrid)

Mohamed Salah (Misri, Liverpool)

Virgil van Dijk (Uholanzi, Liverpool)

MCHEZAJI BORA – WANAWAKE:

Lucy Bronze (Uingereza, Manchester City)

Delphine Cascarino (Ufaransa, Lyon)

Caroline Graham Hansen (Norway, Barcelona)

Pernille Harder (Denmark, Chelsea)

Jennifer Hermoso (Uhispania, Barcelona)

Ji So-yun (Korea Kusini, Chelsea)

Sam Kerr (Australia, Chelsea)

Saki Kumagai (Japan, Lyon)

Dzsenifer Marozsan (Ujerumani, Lyon)

Vivianne Miedema (Uholanzi, Arsenal)

Wendie Renard (Ufaransa, Lyon)

KOCHA BORA – WANAUME:

Marcelo Bielsa (Argentina, Leeds United)

Hans-Dieter Flick (Ujerumani, Bayern Munich)

Jurgen Klopp (Ujerumani, Liverpool)

Julen Lopetegui (Uhispania, Sevilla)

Zinedine Zidane (Ufaransa, Real Madrid)

KOCHA BORA – WANAWAKE:

Lluis Cortes (Uhispania, Barcelona)

Rita Guarino (Italia, Juventus)

Emma Hayes (Uingereza, Chelsea)

Stephan Lerch (Ujerumani, Wolfsburg)

Hege Riise (Norway, LSK Kvinner)

Jean-Luc Vasseur (Ufaransa, Lyon)

Sarina Wiegman (Timu ya taifa ya Uholanzi)

You can share this post!

Morans wang’atwa na ‘The Lions’ ya Senegal mechi za...

Corona yasukuma milioni 2 kwa dhiki