• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Jinsi mafuriko yanavyoathiri shule zilizoko katika mitaa ya mabanda Nairobi

Jinsi mafuriko yanavyoathiri shule zilizoko katika mitaa ya mabanda Nairobi

Na SAMMY KIMATU

[email protected]

SHULE nne katika mitaa ya mabanda ya Mukuru katika Kaunti ya Nairobi zitafungwa ikiwa serikali haitachukua hatua ya haraka kuzuia mafuriko yaliyosumbua kwa zaidi ya miaka mitano.

Shule hizo zinaathiriwa na mafuriko kila mwaka kutokana na unyakuzi wa ardhi katika kingo za mto Ngong.

Shule zilizoathirika ni pamoja na Shule ya Msingi St Bakhita, Shule ya Upili ya St Michael, Shule ya Upili ya Viwandani na shule ya msingi ya St Elizabeth.

Shule hizo nne ziko katika kaunti ndogo ya Makadara. Aidha, wanayakuzi wa ardhi ambao humwaga mchanga ndani ya mto na kulazimisha maji kupita kuelekea shuleni baada ya kujenga nyumba na vibanda katika kingo za mto.

“Mara tu wanapotupa tani za mchanga kwenye kingo za mto, maji husukumwa kuelekea shuleni. Hata baada ya shule hizo kulalamikia idara husika, hakuna hatua iliyochukuliwa, ’’ mwalimu mmoja ambaye hakutaka kutajwa katika vyombo vya habari alisema. Jitihada kali za bodi ya usimamizi wa shule hazijazaa matunda baada ya kuripoti kwa serikali ya kaunti ya Nairobi na Mamlaka ya Kutunza Mazingira Nchini (NEMA).

Jumatano, Taifa Leo iliona ukuta wa shule katika Shule ya Msingi ya St Elizabeth baada ya ukuta wa awali kuanguka kwa sababu ya mafuriko.

Ukuta wa shule katika Shule ya Msingi ya St Elizabeth. Picha/ Sammy Kimatu

Mwaka 2019 mafuriko yalilazimisha zaidi ya wanafunzi 1,300 katika shule hiyo kukaa nyumbani. Kina cha kilikuwa takribani futi nne katika eneo yoye ya shule.

“Kila mwaka, tunalazimika kuwarudisha wanafunzi nyumbani kwa sababu maji hujaa kote shuleni huku nayo masomo yakivurugwa,” mwalimu mmoja wa Shule ya St Elizabeth akaeleza.

Kufuatia mafuriko, shule zinakabiliwa na gharama za ziada pia. Vivyo hivyo katika shule ya upili ya St Bakhita na St Michael, mambo sio tofauti.

Wafanyakazi walikuwa na shughuli nyingi wakijenga vizuizi vya maji nje ya ua la shule hizo ili kuzuia maji kuharibu ukuta baada ya wafanyabiashara kando ya Mto Ngong uliotamba kutoka barabara ya Likoni katika sehemu kati ya Daraja la Express kuelekea mtaa wa mabanda wa Mukuru-Maasai.

Mabwanyenye wamejenga nyumba za kukodisha na yadi za wafanyabiashara wa juakali zilizojengwa juu ya mchanga.

Mto umegeuzwa na kulazimisha maji kuelekea ukuta wa shule hizo mbili.

You can share this post!

Uhuru aelezea matumaini ya BBI ‘kusuluhisha...

Lewandowski aongoza Bayern kupepeta Salzburg 3-1 na kufuzu...