• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
KCB yalenga kutikisa msimu mpya kuingia mashindano ya CAF

KCB yalenga kutikisa msimu mpya kuingia mashindano ya CAF

Na GEOFFREY ANENE

WANABENKI wa KCB wanalenga kuwa katika orodha ya klabu zitakazopeperusha bendera ya Kenya kwenye mashindano ya Shirikisho la Soka barani Afrika (CAF) msimu 2021-2022.

Kutimiza azma hiyo, kocha Zedekiah ‘Zico’ Otieno amesema Alhamisi kuwa KCB itajituma vilivyo katika msimu mpya wa 2020-2021 ili ipate tiketi kwa kushinda Ligi Kuu ama kubeba Kombe la Shirikisho la Soka Kenya (FKF Cup).

Mshindi wa Ligi Kuu huingia Klabu Bingwa Afrika naye bingwa wa FKF Cup hufuzu kuwakilisha nchi katika Kombe la Mashirikisho Afrika (Confederation Cup).

“Tumekuwa tukifanya mazoezi tukifuata masharti yaliyowekwa na wizara za Afya na Michezo ya kudhibiti maambukizi ya virusi vya corona. Lengo letu msimu huu ni kushinda Ligi Kuu. Tusiponyakua taji la ligi, basi tutajikakamua kuibuka mabingwa wa Kombe la FKF. Tunataka kuwakilisha Kenya katika mashindano ya Afrika na hakuna njia nyingine ya kufanya hivyo isipokuwa kushinda mashindano hayo,” Otieno alisema Alhamisi baada ya kuongoza vijana wake kutitiga Kibera Black Stars 3-0 katika mechi ya kupimana nguvu uwanjani Ruaraka.

Kocha huyo aliongeza kuwa KCB iko tayari kwa msimu mpya.

Amejawa imani kuwa vijana wake wanaweza kufanya ndivyo baada ya kupoteza 2-1 dhidi ya Bandari katika mechi yao ya mwisho kabla ya ligi kusitishwa ghafla kutokana na mkurupuko wa virusi vya corona mwezi Machi.

Wakati wa kusimamishwa kwa ligi hiyo mwezi Machi, KCB ilikuwa katika nafasi ya tano baada ya kuzoa alama 41.

KCB imeratibiwa kufungua msimu mpya dhidi ya mabingwa wa mwaka 2009 Sofapaka uwanjani Kenyatta mjini Machakos mnamo Novemba 29. Itamenyana na Nairobi City Stars uwanjani Nyayo mnamo Desemba 4 kabla ya kufunga mwaka 2020 dhidi ya Kakamega Homeboyz mnamo Desemba 12.

Wanabenki wa KCB hawajawahi kushinda ligi. Baadhi ya wapinzani wao wakuu katika kampeni ya msimu mpya ni mabingwa wa mataji 19 Gor Mahia na washindi wa zamani AFC Leopards, Tusker, Sofapaka, Mathare United na Ulinzi Stars. Washiriki wengine kwenye ligi hiyo ni Homeboyz, Kariobangi Sharks, Zoo, Nzoia Sugar, City Stars, Bidco United, Vihiga United, Posta Rangers, Western Stima, Bandari na Wazito.

You can share this post!

Lewandowski aongoza Bayern kupepeta Salzburg 3-1 na kufuzu...

Wahudumu wa tuktuk Githurai wakarabati barabara mbovu...