• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
TZ yararua Somalia bila huruma Cecafa ikipamba moto

TZ yararua Somalia bila huruma Cecafa ikipamba moto

Na GEOFFREY ANENE

MABINGWA watetezi Tanzania wamefuzu kushiriki nusu-fainali ya mashindano ya soka ya Afrika Mashariki na Kati (Cecafa) kwa wachezaji wasiozidi umri wa miaka 20 baada ya kunyeshea Somalia 8-1 mjini Arusha, Alhamisi.

Ngorongoro Heroes, ambao walikung’uta 6-1 katika mechi ya Kundi A na ya kufungua mashindano haya mnamo Novemba 20, walizamisha Somalia kupitia mabao ya Abdul Hamisi Suleiman dakika ya tatu, Ben Sarrkie (14), nahodha Kelvin Pius John (25, 33, 60), Kassim Haruna (47), Frank George (65) na Anuar Jabir (86). Somalia ilikuwa imesawazisha 1-1 kupitia mchezaji Sahal Muhamed dakika ya sita kabla ya kusambaratishwa kabisa.

Ijumaa itakuwa zamu ya Rising Stars ya Kenya dhidi ya Sudan katika mechi ya Kundi C. Stars ya kocha Stanley Okumbi ilianza kampeni yake kwa kucharaza Ethiopia 3-0 Novemba 23. Sudan ilipigwa 3-2 na Ethiopia katika mechi yake ya kwanza hapo Novemba 25 kwa hivyo mechi ya Ijumaa inatarajiwa kuwa moto.

Mshindi wa kundi C pia ataungana na Tanzania ambayo imeonyesha mapemamapema kuwa haitakubali taji litoke nchini humo. Kenya na Sudan zilikutana mara mbili jijini Nairobi katika mechi za kirafiki majuma matatu yaliyopita ambapo Stars waliibuka washindi kwa jumla ya mabao 5-2.

Uganda Hippos iko pazuri kufuzu kushiriki nusu-fainali kutoka Kundi B baada ya kulipua Burundi 6-1 Novemba 25. Hippos ilitoka 0-0 dhidi ya Sudan Kusini katika mechi yake ya ufunguzi. Mshindi wa mashindano haya atajikatia tiketi ya kuwa nchini Mauritania kwa Kombe la Afrika la Under-20 mwaka 2021.

RATIBA NA MATOKEO:

Kundi A

Tanzania 6-1 Djibouti (Novemba 22)

Djibouti 2-1 Somalia (Novemba 24)

Somalia 1-8 Tanzania (Novemba 26)

Kundi B

Sudan Kusini 0-0 Uganda (Novemba 23)

Uganda 6-1 Burundi (Novemba 25)

Burundi na Sudan Kusini (Novemba 27)

Kundi C

Ethiopia 0-3 Kenya (Novemba 23)

Sudan 2-3 Ethiopia (November 25)

Kenya na Sudan (Novemba 27)

Nusu-fainali

Mshindi Kundi B na Mshindi Kundi C (Novemba 30)

Mshindi kundi A na timu iliyomaliza mechi za makundi ya pili kwa alama nyingi (Novemba 30)

Mechi ya kupata nambari tatu na nne (Desemba 2)

Fainali (Desemba 2)

  • Tags

You can share this post!

Faith Kipyegon kuacha mbio za mita 1,500 na kuhamia mbio za...

Raila afafanua kuhusu mkanganyiko kwenye hotuba yake