• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 9:15 PM
CHOCHEO: Usiwe zuzu wa mapenzi

CHOCHEO: Usiwe zuzu wa mapenzi

Na BENSON MATHEKA

“HUWEZI ukamfanya mtu mwingine kuwa bora usipojiboresha kwanza. Huwezi ukapata mpenzi unayemtamani usipotia bidii ya kufanya utamaniwe.” Huu ndio ushauri ambao Jimi huwa anakumbuka kila siku katika safari na maisha yake ya mapenzi.

Barobaro huyu anaamini kwamba japo hakuna mtu mkamilifu katika ulimwengu wa mapenzi, ili mtu apate mwanadada wa ndoto yake wa kuoa, ni sharti atie bidii kujiimarisha.

“Nilikuwa nimevunjika moyo kwa sababu ya kukosa mchumba hadi nilipokutana na wataalamu wa masuala ya mapenzi. Walinidadisi sana kuhusu aina ya mpenzi ninayesaka. Niliwaeleza natamani demu aliye na ajira, aliyejitunza, mcha Mungu na aliye na maono ya siku zijazo. Waliniambia kwamba mkunwa hujikuna na ninaweza kupata demu wa aina hiyo nikitimiza hayo kwanza,” asema Jimi.

Baada ya kupatiwa ushauri huu, aliutilia maanani na akajitahidi kwa kila hali. Alirudi chuo kikuu kuongeza masomo, akapata kazi katika benki, akanunua gari na akashikilia kwa dhati imani yake kwa Mungu hadi alipompata Irene, meneja wa shirika moja la kimataifa ambaye alikuwa na maono sawa na yake. Irene anasema alivutiwa na Jimi kwa sababu amejipanga katika maisha.

“Ni mcha Mungu kama mimi na anajua anachotaka maishani. Kama ni pesa niko na zakutosha. Jimi sio kama wanaume wanaotamani wanawake walio na pesa ilhali wao hawataki kuzitafuta. Nilipompata, maisha yetu yalikamilika na tunafurahia ndoa yetu,” asema.

Vigezo

Wataalamu wa masuala ya mapenzi wanasema njia ya pekee ya kupata mpenzi wa ndoto yako ni kuhakikisha unatimiza vigezo unavyotaka awe navyo. “Jitengeneze kwanza, jiandae kwanza. Jikarabati na ukarabati maisha yako. Ukitaka mpenzi aliye na gari, tia bidii ununue lako. Huwezi ukamtunza mtu ikiwa huwezi kujitunza binafsi,” asema Harry Okoth, mwanasaikolojia wa shirika la Life Beyond Today.

Kulingana na Harry, watu hujisononesha kwa kuwamezea mate watu ambao tayari wamefanikiwa ilhali wao hawataki kutia bidii kufanikiwa. “Siku hizi wanaume pia wanataka wanawake waliofanikiwa. Badala ya kuhangaika, tia bidii kujenga maisha yako na utawapata. Ukitaka mke au mume mcha Mungu, muogope Mola pia,” asema.

Cecilia Mathenge wa shirika la Center That Hold jijini Nairobi, anasema watu huwa wanakosea kwa kuamini kuwa wanaweza kubadilisha wenzao kuwa bora wakianza uhusiano wa kimapenzi. “Hauwezi ukabadilisha mtu asiyeweza kujibadilisha. Wale waliojaribu kufanya hivyo waliishia kujuta,” asema.

Eve Nekesa mkazi wa mtaa wa Umoja, Nairobi, anasema kwamba alijuta kufikiri kuwa angembadilisha mwanamume mlevi aliyevutiwa naye. “Haikuwezekana, nilijuta kwa kuchukua uamuzi huo. Jamaa hakuwa na maono na alidhani kila hatua niliyochukua kumfanya abadilike ilikuwa ya kumdhalilisha,” asema.

Mwanadada huyu asema baada ya kuachana na jamaa huyo alizingatia biashara yake na kushikilia imani yake katika Mungu hadi akampata Edu, mtaalamu wa masuala ya uwekezaji na sasa wanapanga harusi.

“Nilichojifunza ni kuwa mtu anafaa kujiimarisha kwanza kabla kusaka mpenzi wa kumfanya kuwa bora. Asiyeshughulika kujiboresha hawezi kumfanya mwingine kuwa bora,” asema.

Cecilia anasema ni makosa kuingia katika uhusiano wa mapenzi kwa kuhisi kuwa umechelewa. “Kuna watu waliofanikiwa maishani ambao hupoteza maono yao na kuanza uhusiano wa mapenzi na watu kwa kuhisi wamechelewa. Uamuzi kama huu ni hatari kwa kuwa unasambaratisha maono yako na kukufanya ujute baadaye. Utulivu, subira na umakini ni muhimu sana katika kupata mpenzi wa ndoto yako,” asema.

Hilda, mfanyakazi wa kampuni moja mjini Athi River, anakubaliana na kauli hii akisema alilazimika kumtema mwanamume aliyemrudisha nyuma kwa kukosa maono. “Nilikutana naye nikiwa na duka. Badala ya kunishika mkono alikuwa akichukua pesa za biashara kwenda kulewa. Sikumvumilia katu, nilimpiga teke haraka upesi,” asema.

You can share this post!

TAHARIRI: Klabu zetu zijiimarishe barani

Sonko amejihami vilivyo kuokoa kazi yake isimtoke