Dimba

Aliyekuwa refarii wa Fifa Said Ali aaga dunia

Na ABDULRAHMAN SHERIFF June 19th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

UMATI wa wanaspoti ulihudhuria mazishi ya aliyekuwa refarii wa kimataifa (Fifa), Said Ali aliyeaga dunia mjini Mombasa Jumatano na kuzikwa katika makaburi ya Waislamu ya Tangana siku hiyo.

Marehemu Ali, mmoja wa waliokuwa waamuzi wachache waliomiliki beji ya Fifa kutoka Kanda ya Pwani aliaga dunia baada ya kuugua ugonjwa wa kupooza (stroke). Alifanyiwa maombi ya mwisho katika Msikiti wa Ibrahim kabla ya kuzikwa makaburi ya Tangana.

Marehemu aliacha mjane na watoto wanne, watatu wa kiume na mmoja wa kike.

Mwakilishi wa Pwani katika Kamati Kuu ya Shirikisho la Soka nchini (FKF), Gabriel Mghendi na Mwenyekiti wa FKF tawi la Kaunti ya Mombasa, Alamin Ahmed ni miongoni mwa viongozi wa soka waliotuma risala za rambirambi kwa familia ya marehemu.

Katika risala yake, Mghendi amesema Ali alikuwa refarii aliyesifika sio kusimamia mechi za timu za kanda hiyo pekee bali hata mechi za Ligi Kuu na hasa zilizohusisha mahasimu wa jadi AFC Leopards na Gor Mahia.

“Ali alipendwa hata aliposimamia mechi za kimataifa,” akasema.

Naye Ahmed amesema marehemu alikuwa kielelezo kizuri kwa waamuzi wanaoinukia ambao mbali na kuwa hawakumuona akichezesha, sifa zake zimekuwa zikiwavutia na kutaka kufikia viwango vya kuwafanya nao wapate beji za Fifa.

Aliyekuwa refarii, Awadh Barafa alisema alivutiwa kujiunga na urefarii kutokana na kusisistizwa na marehemu.

“Nilipenda kuwa mpiga kipenga kutokana na kuambiwa na Ali na nilijifunza mengi kutoka kwake,” akasema Barafa.

Miongoni mwa waamuzi wachache kutoka Pwani waliopata kuwa na beji ya Fifa ni Dick Simiyu, Khamis Baghazally, Miraj Abdalla, Gharib Suleiman na marehemu Gabriel Ngesa.

Ali aliwahi kuwa mchezaji wa Leeds United FC na nduguye marehemu Badi Ali aliyekuwa mchezaji wa timu ya taifa ya Kenya na Mwenge na marehemu Khamis Ali ambaye pia alikuwa refarii na marehemu Rashid Ali aliyekuwa mwanasoka wa Chelsea FC.

Mnamo wiki iliyopita, aliyekuwa mchezaji wa Mwenge (Liverpool), Abdul Swaleh almaarufu Pele aliaga dunia. Marehemu aliswaliwa msikiti wa Marembo na kuzikwa makaburi ya Waislamu ya Kikowani.