Ambani, Mutokah wabakia farasi wawili vita vya kuongoza AFC Leopards
VITA vya kuwania kiti cha mwenyekiti wa AFC Leopards vimebakia baina ya aliyekuwa mshambuliaji wa kimataifa Bonface Ngairah Ambani na aliyekuwa Mkurugenzi wa Biashara wa klabu hiyo, Enos Vincent Mutokah.
Hii ni baada ya aliyekuwa afisa mkuu wa klabu hiyo, Ronald Namai kujiondoa kwenye vita hivyo na kuamua kumuunga mkono Ambani ambaye pia alikuwa mshambuliaji matata wa klabu hiyo ya Ingwe pamoja na timu ya taifa ya Harambee Stars.
Wawili hao wameidhinishwa na Tume ya Uchaguzi nchini (IEBC) kupigania kiti hicho hapo Juni 29, 2025 ambapo mshindi atamrithi mwenyekiti wa sasa, Dan Shikanda ambaye hakubaliwi kutetea wadhifa huo baada ya kuhudumu kwa mihula miwili kwa kipindi cha miaka sita kuanzia 2019.
Tayari Shikanda ameahidi kuachilia mamlaka kwa atakayechaguliwa kati ya wawili hao wanaotoka Kaunti ya Kakamega, Magharibi mwa Kenya.
Walioidhinishwa kupigania kiti cha Katibu-Mkuu ni Robert Khamala Situma Omusawa, Isaac Mulanda Mulindi na Irene Sitawa Wekesa maarufu kama Renee baada ya Asava Kadima na Dennis Esikuri Njaka kuiondoa kwenye kinyang’anyiro hicho.
Watatu hao watakuwa wakiwania nafasi ya kujaza nafasi ya Gilbert Andugu aliyefariki na kuzikwa mwezi uliopita kutokana na maradhi ya muda mrefu.
Uadhifa huo unashikiliwa na mwanakamati Caroline Walusaga.
Watakaopigania uadhifa wa mweka hazina ni Patrick Kanyangi Logedi, Edward Chamwata Buhasho na Newton Lime Luchacha.
Oliver Napali anayeshikilia kiti hicho amesema hajakitetea kutokana na sababu za kiniafsi.
Mbali na kuchezea Leopards na Harambee, vilevile Ambani alikisakatia Yanga nchini Tanzania, Tusker FC kabla ya kuenda majuu kusakata soka ya kulipwa nchini India na Milki za Kiarabu.
Pamoja na nduguye Fred, Ambani alikuwa katika kikosi kilichoshindia Ingwe ubingwa wa mwisho wa ligi kuu mnamo 1998.
Kwenye mafesto yake, mshambuliaji huyo mstaafu alisema ripoti zote za matumizi ya kifedha ya Ingwe itakuwa wazi kwa wanachama huku akiahidi kuzima mbinu zote za watu laghai.
Vile vile ameahidi kuipata timu ya wanawake ya Ingwe usaidizi unaofaa kama udhamini na mavazi ya kutosha.