Dimba

Chebet, Omanyala katika kikosi cha wanariadha 58 wa Kenya watakaonogesha Riadha za Dunia 2025

Na GEOFFREY ANENE July 23rd, 2025 Kusoma ni dakika: 1

BINGWA wa Riadha za Dunia mwaka 2015, Kenya, imetangaza orodha ya wanariadha 58 watakaopeperusha bendera yake kwenye makala ya 20 yatakayofanyika mjini Tokyo, Japan, mnamo Septamba 13-21.

Shirikisho la Riadha Kenya (AK) lilitoa orodha hiyo baada ya mchujo wa kuchagua timu ya taifa uliofanyika Ulinzi Sports Complex, Nairobi, hapo Jumanne.

Shirikisho hilo pia lilitangaza washiriki wa mbio za kilomita 42 ambao ni Peris Jepchirchir, Jackline Cherono, Magdaline Masai, Vincent Ngetich, Erick Sang na Kennedy Kimutai. Vivian Cheruiyot na Hillary Kipkoech wanasubiri atakayekosa kwa sababu ya jeraha ama kujiondoa.

Lilian Odira (kati), Sarah Moraa (kushoto) na Vivian Chebet Kiprotich wakishiriki 800m kwenye mchujo huyo katika uga wa Ulinzi Sports Complex, Nairobi. PICHA | CHRIS OMOLLO

Mshikilizi wa rekodi ya Afrika na bingwa wa Michezo ya Jumuiya ya Madola Ferdinand Omanyala ndiye matumaini yote katika mbio za mita 100. Mary Moraa atetea taji lake la dunia la 800m naye bingwa wa 1,500m na 5,000m Faith Kipyegon amepewa fursa ya kuwania kuhifadhi mataji hayo.

Washilikizi wa rekodi za dunia Beatrice Chebet (5,000m na 10,000m) na Agnes Ngetich (10km barabarani) walitajwa katika vitengo vya 5,000m na 10,000m.

Mfalme wa Olimpiki 800m Emmanuel Wanyonyi, mshikilizi wa rekodi ya dunia ya chipukizi wasiozidi umri wa miaka 20 wa 1,500m Phanuel Koech, makinda Faith Cherotich na Edmund Serem (3,000m kuruka viunzi na maji) pia wamo kikosini.

Nicholas Kebenei ashinda 800m kwenye mchujo huo. PICHA | CHRIS OMOLLO

Bingwa wa dunia wa kurusha mkuki mwa 2015 na pia mshikilizi wa rekodi ya Afrika, Julius Yego, ni mwakilishi wa Kenya katika fani za uwanjani. Vikosi vya wanaume kupokezana vijiti vya 4x100m na 4x400m pamoja na mbio mseto za 4x400m pia vilitajwa jana.

AK ilisema kuwa wanariadha Alex Ngeno (800m), Brian Komen (1,500m), na Celestine Biwot na Geoffrey Kirwa (3,000m kuruka viunzi na maji) wanaweza kupata tiketi kutoka kwa riadha za Diamond League.

Mrushaji mkuki Irene Jepkemboi na mshiriki wa fani ya kuruka utatu (triple jump) Winny Bii wanasubiri kipindi cha kufuzu kifungwe ili kujua hatima yao.