Dimba

Chelsea walazimika kutambua Arsenal ni ‘mkubwa wao’ kwa sasa

Na MASHIRIKA February 4th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WINGA wa Arsenal Eze Eberechi amesema ni ndoto yake kushinda mataji na Arsenal akisema tayari anawazia fainali itakayogaragazwa katika uga wa Wembley baada The Gunners kufuzu kwa fainali ya Carabao Jumanne usiku.

Nguvu mpya Kai Havertz alifunga bao katika dakika ya mwisho na kuisaidia Arsenal kutia kapuni ushindi wa 1-0 kwenye mechi ya mkondo wa pili ugani Emirates.

Arsenal ilishinda mechi ya mkondo wa kwanza 3-2 na ilifuzu kwa fainali kwa jumla ya mabao 4-2. Fainali hiyo itagaragazwa mnamo Machi 22 kwenye uwanja wa kihistoria wa Wembly.

Vijana wa Mikel Arteta huenda wakakutana na Manchester City au Newcastle ambazo zilikuwa zicheze nusu fainali nyingine baadaye jana usiku. City walishinda mechi ya mkondo wa kwanza 2-0 dhidi ya Magpies.

“Arsenal imekuwa klabu yangu tangu utotoni na imekuwa ndoto yangu kushinda mataji nao. Naamini tuna kikosi kizuri ambacho kikipambana vizuri basi tuna nafasi ya kutwaa ubingwa wa C arabao,” akasema Eze.

Eze alicheza dakika zote 90 katika mechi ya Jumanne huku akiwatatiza mabeki wa Chelsea hasa Marc Cucurella akiwa na wakati mgumu kumdhibiti.

Arsenal ipo pazuri kutwaa mataji msimu huu kwa sababu wapo kileleni mwa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) kwa mwanya wa alama sita, wapo raundi ya nne ya Kombe la FA na pia wameshinda mechi zao zote katika ngarambe ya Klabu Bingwa Ulaya (UEFA).

Fainali ya Carabao ni fahari ya kipekee kwa sababu ndiyo mara ya kwanza baada ya miaka sita ambapo wametinga fainali ya kipute chochote kile.

Nusu fainali ya Jumanne usiku ilikuwa ya tatu ambapo Arsenal imeshiriki katika Carabao baada ya kubanduliwa katika hatua hiyo hiyo mnamo 2022 na 2025.

Kocha wa Arsenal Mikel Arteta aliridhishwa na jinsi vijana wake walivyoishinda Chelsea akisema sasa kibarua ni kufika Wembley na kutwaa Kombe la Carabao.

“Naisubiri sana fainali hiyo kwa sababu tumekuwa tukitia bidii sana ili tufuzu japo hapo awali hatukufanikiwa.

Pia nimefurahi sana jinsi ambavyo mechi ilikamilika na bao ambalo Kai Havertz alifunga,” akasema Arteta alipozungumza baada ya mechi hiyo.

“Hili ndilo kombe la kwanza ambalo tuna nafasi ya kushinda kama klabu msimu huu. Kwa hivyo, tuliendee na tuweke juhudi zote,” akaongeza mkufunzi huyo ambaye pia alisakatia Everton na Arsenal enzi zake akiwa mchezaji.

Licha ya kubanduliwa, Kocha wa Chelsea Liam Rosenior atafurahia mchezo wa timu yake ambao ulionekana kuimarika sana ikilinganishwa na mkondo wa kwanza.

“Ukweli ni kwamba tuliimarika kimchezo kuliko mkondo wa kwanza. Ni uchungu kupoteza nusu fainali kwa sababu tulitaka tusonge mbele. Hata hivyo, tumeimarika na tuzidi kujituma katika mashindano mengine,” akasema Liam.

“Tulikuwa tukipambana tupate goli na mabeki wetu wakaenda kwa kijisanduku cha Arsenal ndiyo maana walipata upenyo na kutufunga,” akaongeza.

Ilipotimia dakika 60 Liam aliwaleta Estevao na Cole Palmer ambao walibadilisha mchezo na kufanya Arsenal ilemewe.

The Gunners walishinda taji la mwisho mnamo 2020 ambapo walishinda Chelsea 2-1 katika fainali ya FA. Mara ya mwisho ambapo walishinda fainali ya Carabao, ni mnamo 2018.

Mwaka huo walipigwa 3-0 na Manchester City na watakuwa na nafasi ya kulipiza kisasi iwapo vijana wa kocha Pep Guardiola watawapiku Newcastle na kutinga fainali.