Chelsea walazimika kutegemea muda wa ziada kupiga limbukeni Wrexham
CHELSEA na Machester City, walijiunga na Arsenal kufuzu robo fainali ya Kombe la Michuano ya FA Jumamosi usiku.
The Blues walitoka nyuma mara mbili na mwishowe wakapata ushindi wa 4-2 dhidi ya Wrexham ya Wales nao City wakawanyorosha wenzao wa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) Newcastle 3-1.
Ilikuwa mechi yenye presha nyingi huku Sam Smith akifungia Wrexham bao la kwanza dakika ya 18 kwa kuutumia vizuri udhaifu wa safu ya ulinzi ya Chelsea.
Lakini wing’a Alejandro Garnacho alilazimisha bao la kujifunga kabla ya mapumziko wakati juhudi zake za kufunga, zilipoondolewa na beki George Thomason na kumpiga mlinda mlango wa Wrexham, Arthur Okonkwo, mgongoni na mpira ukaingia wavuni.
Katika kipindi cha pili, Chelsea ilifanya mabadiliko kadhaa baada ya dakika 45 mbovu, lakini Wrexham walipata tena bao la uongozi dakika ya 78 kupitia Callum Doyle.
Dakika nne baadaye, Chelsea walisawazisha kwa mara nyingine kupitia Josh Acheampong na mechi hiyo ikaishia sare 2-2 na kuelekea muda wa ziada.
Wenyeji hao walipata pigo dakika ya (90+3) wakati George Dobson alipata kadi nyekundu.
Mechi iliendelea hadi dakika za ziada na kombora la Alejandro Garnacho katika muda wa ziada ambalo liliwaweka mbele kwa mara ya kwanza, huku mchezaji wa akiba Joao Pedro akifunga bao la nne.
Chelsea watacheza ugenini dhidi ya PSG Jumatano hii katika hatua ya 16 bora ya Ligi ya Mabingwa.
Katika mechi Ugani St James’ Park, mabao ya Savinho (39), Omar Marmoush na (47, 65) yalitosha kuipa City ushindi dhidi ya Newcastle ambao walipata bao la kufutia machozi kupitia Harvey Barnes (18).
Baada ya mechi hii, Newcastle watakabiliana na Barcelona katika mechi ya kwanza ya hatua ya 16 bora ya Ligi ya Mabingwa katika uwanja wa St James’ Park siku ya Jumanne, kabla ya kusafiri hadi Stamford Bridge.
City nao watasafiri hadi Santiago Bernabeu kuwakabili Real Madrid katika mechi ya kwanza ya hatua ya mwondoano ya Ligi ya Mabingwa Jumatano, kabla ya kucheza na West Ham katika uwanja wa London siku ya Jumamosi mechi ya EPL.
Baadae leo, West Ham itakuwa mwenyeji wa Brentford katika mechi nyingine ya FA.