Guardiola: Arsenal tunawacheki hapa karibu; hawako mbali!
PEP Guardiola sasa amepanga “kukabana koo na Arsenal”, katika mbio za kuwania ubingwa wa Ligi kuu ya Uingereza (EPL).
City walitoka nyuma na kuandikisha ushindi wa 2-1 dhidi ya wenyeji Liverpool Jumapili ugani Anfield. Kiungo Dominik Szoboszlai alicheka na wavu wa kwanza dakika ya 74 kabla ya Bernado Silva kusawazisha dakika ya 84. Erling Halaand alifunga bao la ushindi kupitia penalti dakika za ziada kipindi cha pili.
Baada ya mechi hiyo, Guardiola alitania kuhusu ushindi wao wa mwisho Anfield miaka mitano iliyopita, ambao ulitokea bila mashabiki kutokana na vizuizi vya Covid 19, akisema;
“Tunachoweza kufanya ni kuwakaba Arsenal koo na kuwa nao bega kwa bega. Ikiwa watateleza tutatumia nafasi hiyo,” alisema Guardiola.
Ushindi huo ulimaanisha kuwa, City (nafasi ya pili na alama 50) wako pointi sita tu nyuma ya vinara Arsenal huku mechi 13 zikisalia kuchezwa ikiwa ni pamoja na ziara ya Gunners kwenye Uwanja wa Etihad mwezi Aprili.
Kuhusu ikiwa angepoteza mechi hiyo, alisema; “Bila shaka tungevunjika moyo tungekosa kupata alama zote muhimu. Maswali yote yangekuwa yale yale kuhusu mbio za ubingwa lakini pointi sita ni bora kuliko tisa. Bado ni nyingi ukizingatia jinsi Arsenal walivyo na nguvu katika idara zote.”
Aliongezea akisema, “Mechi 10 za mwisho, kutokana na uzoefu wangu, ni ngumu sana. Jambo muhimu ni kujaribu kuwepo na kuboresha kwa sababu kipindi cha pili hakikuwa kizuri tena.”
Wenyeji walipata pigo dakika ya 13 ya muda wa ziada baada ya Szoboszlai kupata kadi nyekundu. Hili lilitokea baada ya Halaand kupata nafasi ya wazi ya kufunga, baada ya mlinda lango wa Liverpool Alison Becker kuondoka langoni kujumuika na wachezaji wengine uwanjani.
Lakini Halaand alipokuwa mbioni kuhakikisha mpira huo umevuka mstari, alivutwa nyuma na Szoboszlai nje ya kijisanduku, Halaand nae akalipiza kisasi kwa kumvuta Szoboszlai hadi kuanguka.
Mpira ulipita mstari lakini, bao hilo likafutiliwa mbali na Szoboszlai akapata kadi nyekundu.