Gyokeres aota tu Arsenal na Man Utd
VIKTOR Gyokeres ametishia kugoma ili kulazimisha Sporting Lisbon wamwachilie ajiunge na Arsenal au Manchester United.
Gyokeres anaamini ni fursa nzuri ya kujiunga na klabu hizo kubwa kwenye Ligi Kuu ya Uingereza.
Sababu ya kutaka kuchukua hatua hiyo ni kwa sababu Sporting sasa wanaonekana kupiga abautani kwa kutaka kumuuza kwa Sh9.6 bilioni kwa kuongeza bei yake hadi Sh14.7 bilioni, kitu kinachomkera Gyokeres kwa kuwa kinaweza kuzuia wanaommezea mate kumsaini.
Nyota huyo kutoka Uswidi amekuwa akiwaniwa na klabu kadhaa kubwa Ulaya kutokana na weledi wake katika ushambulizi ambao umeshuhudia akifunga mabao 97 katika miaka miwili ambayo amekuwa Ureno ambapo pia ametwaa ubingwa wa Primeira Liga.
Inaaminika Gyokeres hajafurahishwa na jinsi mazungumzo kuhusu uhamisho wake yanajikokota na yuko tayari kufanya mgomo ili kulazimisha uhamisho.
Gyokeres, 27, anaamini Sporting wanafanya uhamisho wake kuwa mgumu na hivyo kumuudhi. Mshambulizi huyo ameweka wazi kuwa anataka kuhama katika kipindi hiki cha uhamisho.
Inasemekana Gyrokeres amefahamisha waajiri wake kuwa hatawachezea tena kwa sababu anahisi kutoheshimiwa na viongozi wa Sporting wanaoonekana kutaka kuvunja ahadi kati yao naye.
Kocha wa Sporting, Rui Borges amekataa kuzungumzia uhamisho wa Gyokeres.
Aidha, ripoti zinadai kuwa mashetani wekundu wa Manchester United, ambao wanaongozwa na kocha wa zamani wa Gyokeres, Ruben Amorim, tayari wamewasilisha ofa wakitafuta kuondoa wanabunduki wa Arsenal kwenye hesabu.
Ilidhaniwa United wangeshindwa kuwania huduma zake baada ya kukosa tiketi ya kushiriki mashindano yote ya Ulaya. Hata hivyo, yasemekana Gyokeres hana tatizo kukosa mashindano ya Ulaya msimu ujao.
Aidha, inaaminika kuwa Gyokeres ametamani kujiunga na Arsenal kutoka mwanzo na kuwa mazungumzo kati ya ajenti wake na wamiliki wa klabu hiyo ya kutoka London Kaskazini yameshika kasi.
United hawajapoteza matumaini ya kusaini Gyokeres, huku ripoti zikidai kuwa Amorim sasa ndiye anaongoza kufanya majukumu ya kumshawishi ahamie ugani Old Trafford.