Man U wadhihirisha hawana nguvu, hawana uwezo wakigura taji la FA
MANCHESTER United walibanduliwa nje ya mashindano ya Kombe la FA Jumapili usiku, baada ya kichapo cha 2-1 dhidi ya Brighton ugani Old Trafford.
Mshambuliaji Danny Welbeck, aliaawadhibu waajiri wake wa zamani kwa kufunga bao la pili na la ushindi dakika ya 64, na kuwapelekea kufuzu kwa raundi ya nne michuano hiyo.
Awali, Brighton walicheka na wavu wa kwanza dakika ya 12 kupitia Brajan Gruda kabla ya Benjamin Sseko kusawazisha mambo dakika ya 85. Dakika nne baadaye, United walipata pigo baada ya nguvu mpya Shea Lacey kupata kadi nyekundu.
Hilo lilikuwa bao la nane la Welbeck dhidi ya United na la sita alipotembelea uwanja aliokuwa akiuita nyumbani katika mashindano yote.

Pia inamaanisha kuwa, kocha wa muda wa United Darren Fletcher sasa amepoteza mechi moja, na kutoka sare ya 2-2 dhidi ya Burnley katika mechi ya Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) wiki jana. Alichukua nafasi ya kocha Ruben Amorim ambaye alitimuliwa tarehe 5 mwezi huu, kutokana na msururu wa matokeo mabaya.
United sasa wameshinda mara moja katika michezo yao saba iliyopita katika mashindano yote, huku Manchester City na Arsenal, wanaowania taji, wakiwa wapinzani wao wawili wanaofuata katika mechi za EPL.
United wanatarajiwa kumtaja kocha mpya wakati wowote wiki hii.
Kocha wa zamani wa United Ole Gunnar Solskjaer na Michael Carrick wametajwa kuwa wagombea wakuu kunoa timu hiyo hadi mwishoni mwa msimu huu.
Katika mechi zingine za FA Jumapili timu, za EPL zilipata ushindi dhidi ya timu za Ligi ya Championship. West Ham United waliinyorosha Queens Park Rangers (QPR), Sheffield United wakawazaba wenzao wa Championship Mansfield Town 4-3.
Leeds United nao wakawanyeshea Derby County 3-1. West Brom United walifuzu baada ya kuwaadhibu wenzao wa Championship 6-5 kupitia matuta ya penalti baada ya mechi hiyo kuishia sare ya 2-2 muda wa kawaida.
Katika mechi nyingine Jumanne, Newcastle United itamenyana na Manchester City katika mkondo wa kwanza wa nusu fainali ya Kombe Carabao Ugani St James’ Park.
Pande hizo mbili zilikutana EPL mwanzoni mwa msimu huu, na Magpies walibuka na ushindi wa 2-1. Kufuzu raundi hii, Newcastle iliishinda Bournemouth kwa penalti 7-6 baada ya sare ya 3-3 muda wa kawaida, huku City ikiizaba Exeter City 10-1.
Kuelekea mechi hii, Newcastle wameshinda mara mbili na kutoka sare mechi moja kati ya sita za awali za Kombe la FA dhidi ya Man City.