Dimba

Man Utd yasoma mgongo wa Aston Villa baada ya ushindi

Na MASHIRIKA February 24th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

LONDON, UINGEREZA

MSHAMBULIAJI Benjamin Sesko alitokea benchi tena na kuokoa Manchester United isitoke sare tasa na Everton, na kuongeza msururu wao kutopoteza mechi 10 katika Ligi Kuu ya Uingereza (EPL).

Sesko, 22, raia wa Slovenia alifunga bao hilo dakika ya 71 likiwa bao lake la tatu akitokea benchini, baada ya kufanya hivyo dhidi ya Fulham na West Ham mara ya mwisho.

Ushindi wa Manchester United umewaweka katika nafasi ya nne kwa alama 48, mbili tu nyuma ya nambari tatu Aston Villa baada ya mechi 27.

Arsenal inaongoza jedwali kwa alama 61, tano mbele ya Manchester City.

Kwa bao hilo, sasa Sesko ndiye mchezaji wa pekee wa EPL kutokea benchi na kufunga mabao mengi (matatu) msimu huu.

Wachezaji wote watatu kati ya waliosajiliwa na Man United mwanzoni mwa msimu huu walihusika katika ufungaji wa bao hilo.

Bryan Mbeumo alipokea pasi ndefu kutoka kwa Matheus Cunha na akammegea Sseko pasi ambayo ilizalisha bao.

Katika mechi hii, timu zote mbili zilikosa ubora, lakini macho yalikuwa kwa United, ambao walikuwa wanatafuta ushindi baada ya Chelsea kupoteza pointi mbili dhidi ya Burnley mnamo Jumamosi katika mbio za kuwania nafasi ya kucheza Ligi ya Mabingwa msimu ujao.

Mlinda lango wa United Senne Lammens alitajwa kama mchezaji bora wa mchezo huo baada ya kuokoa mashuti manne makali.

“Hatukuwa katika ubora wetu, nadhani tunapaswa kuwa bora zaidi. Tangu meneja ameingia tumekuwa tukifanya kazi vizuri sana pamoja,” alisema Lammens.

Kuhusu Sesko kocha wa United Michael Carrick alisema, “Tumekuwa na mazungumzo mazuri sana. Atakuwa mchezaji muhimu kwetu kwa muda mrefu, nina hakika juu ya hilo. Tunapaswa kudhibiti hilo. Tuna wachezaji wazuri wa ushambuliaji. Amefanya tofauti kubwa kwetu anapokuwa uwanjani.”