Dimba

Mwanasoka Masoud Juma afunguka kuhusu wake zake wawili

March 16th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MSHAMBULIAJI wa Kenya Masoud Juma amefunguka kuhusu maisha yake ya kifamilia na mipango yake ya baadaye, akithibitisha kuwa ana wake wawili huku akisema familia yake imekuwa nguzo muhimu katika maisha yake ya kibinafsi na taaluma ya soka.

Akizungumza kwenye kipindi cha Football 90 kinachoendeshwa na mwanahabari Mike Okinyi katika kituo cha Citizen TV, Juma alisema amekuwa na mke wake wa pili kwa miaka saba sasa.

Alieleza kuwa licha ya kuwa mwanasoka wa kulipwa nje ya nchi, wake zake wamekuwa wakimuunga mkono na kuhakikisha familia yao inaendelea kuwa na umoja.

“Familia yangu imekuwa msaada mkubwa sana. Wake zangu wamenipa nguvu sana hasa ninapokuwa ughaibuni nikicheza soka ya kulipwa,” alisema Juma.

Mwanasoka huyo hivi majuzi alikuwa akicheza soka ya kulipwa katika klabu ya Nejmeh SC inayoshiriki Ligi Kuu ya Lebanon na yenye makao yake katika jiji la Beirut.

Alijiunga na klabu hiyo mwaka 2025 na hata kufunga bao katika mechi yake ya kwanza, hatua iliyomfanya kuanza kujizolea umaarufu miongoni mwa mashabiki wa timu hiyo.

Hata hivyo, Juma kwa sasa yuko nchini baada ya shughuli za soka kusitishwa nchini Lebanon kutokana na mvutano wa kivita katika eneo la Mashariki ya Kati uliosababisha kusimamishwa kwa mechi za ligi hiyo kwa muda.

Amesema anatumia kipindi hiki kufanya mazoezi na klabu ya Kuta Collection FC huku akisubiri hali huko Mashariki ya Kati

Aidha, Juma alifichua kuwa hapo awali alikuwa na wazo la kuwania kiti cha ubunge katika siku zijazo, lakini kwa sasa ameahirisha mpango huo baada ya kufanya mashauriano na familia yake.

Alisema uamuzi huo ulilenga kumpa muda zaidi kuangazia taaluma yake ya soka, akisisitiza kuwa familia yake ndiyo msingi wa maamuzi mengi anayofanya maishani.