Dimba

Riadha za Kitaifa: Omanyala ang’ara 100m, Oketch wa KDF wembe 400m

Na GEOFFREY ANENE June 28th, 2025 Kusoma ni dakika: 4

MASTAA Ferdinand Omanyala, Zablon Ekwam, Lilian Odira na Mercy Oketch ni baadhi ya wanariadha waliotikisa kwenye Riadha za Kitaifa za Kenya zilizokamilika baada ya siku mbili ugani Ulinzi Sports Complex mjini Nairobi, Ijumaa.

Afisa wa polisi Ferdinand Omanyala aliibuka mshindi katika mbio za mita 100 anazopenda kwa sekunde 10.08 akifuatiwa na wanajeshi Steve Onyango (10.27) na Meshack Babu (10.31) pamoja na chipukizi Clinton Aluvi wa Polisi (10.48).

Aluvi yuko katika timu ya Kenya itakayoshiriki Riadha za Afrika za Under-18 na Under-20 nchini Nigeria mwezi ujao. Ameonyesha matumaini makubwa kwa kuimarisha muda wake bora kutoka 10.61 hadi 10.48. Ndugu mdogo wa Omanyala, Isaac Omurwa kutoka timu ya Vyuo Vikuu, alikamata mkia kwa 14.39.

George Mutinda (kulia) wa Polisi akimaliza mbele ya Kevin Kipkorir mbio za 400m wakati wa mashindanohayo. PICHA | CHRIS OMOLLO

George Mutinda (44.51) na Brian Tinega (44.67) pia kutoka Idara ya Polisi na Kelvin Kipkorir (44.80) kutoka Idara ya Magereza walifagia nafasi tatu za kwanza katika kitengo cha 400m wakitinga muda wa kufuzu kwa Riadha za Dunia nchini Japan baadaye Septemba mwaka huu – wa sekunde 44.85.

Esther Mbagari kutoka Magereza alitwaa umalkia wa 100m kwa sekunde 11.89 akifuatiwa na Loice Morara wa Kikosi cha Ulinzi (KDF) kwa sekunde 12.00 na Diana Aoko wa Nyanza North (12.05) katika nafasi tatu za kwanza.

Gladys Ngure wa Magereza alitawala 100m kuruka viunzi kwa sekunde 14.53 mbele ya Philian Kerubo wa KDF (15.28) na Veronica Chebet kutoka Polisi (15.42).

Wiseman Were wa KDF alitawazwa mfalme wa 110m kuruka viunzi alipotumia sekunde 14.11 kuibuka kidedea. Alifuatiwa na mwanajeshi mwenzake William Mbevi (14.78) na Godwin Ochieng wa KATTI (15.50).

Millecent Ndoro kutoka Polisi alinyakua taji la 200m kwa sekunde 23.82 akifuatiwa na Mbagari wa Magereza (24.08) na Morara kutoka KDF (24.13).

Nafasi tatu za kwanza za kitengo cha wanaume 200m ziliwaendea Ekwam wa KDF kwa sekunde 20.47, Omanyala (20.53) na Dennis Mwai kutoka Polisi (20.73).

Taji la kinadada la 400m lilinyakuliwa na mshikilizi wa rekodi ya kitaifa Oketch kutoka KDF aliyetumia sekunde 50.32. Alifuatiwa kwa karibu na afisa wa polisi Mercy Chebet (51.80) na mwanajeshi mwingine Lanoline Aoko (51.81).

Rahab Ndirangu kutoka Polisi aliponyoka na taji la 400m kuruka viunzi kwa sekunde 58.87 mbele ya Ngure (60.66) na mwanajeshi Sherah Chepkorir (60.92).

Mbali na 110m kuruka viunzi, Were pia aliwika 400m kuruka viunzi akiibuka mshindi kwa sekunde 49.29 mbele ya Cyrus Kipkemboi wa KATTI (49.66) na Peter Kithome wa Southern (50.97).

Malkia wa Riadha za Dunia 800m, Mary Moraa kutoka Polisi, alishinda nusu-fainali yake katika mbio hizo za kuzunguka uwanja mara mbili, lakini hakujitokeza kwa fainali ambayo Odira wa Magereza alitawala kwa dakika 2:02.08 akifuatiwa na Sarah Moraa wa Polisi (2:02.56) na Judy Kemunto wa South Rift (2:02.56).

Kanda ya Western ilijifariji na dhahabu ya 800m ya wanaume kupitia kwa Kelvin Loti aliyeimarisha muda wake bora kutoka dakika 1:44.07 hadi 1:43.61. Alimaliza mbele ya Laban Chepkwony wa KDF (1:43.64) na Alex Ng’eno wa Magereza (1:45.55). Nyota Noah Kibet wa Polisi na Ferguson Rotich wa kanda ya South Rift hawakuwa na lao wakimaliza nambari tano na sita mtawalia.

Mercy Oketch wa KDF akishinda 400m. PICHA | CHRIS OMOLLO

Mary Nyaruai wa Polisi, Teresia Gateri kutoka kanda ya Central na Vivian Chebet wa KDF walikamata nafasi tatu za kwanza za 1,500m za kinadada kwa dakika 4:09.68, 4:10.10 na 4:11.30 mtawalia.

Nafasi tatu za kwanza katika kitengo cha wanaume cha mbio hizo za kuzunguka uwanja mara nne zilinyakuliwa na wakali Reynold Cheruiyot wa Polisi kwa dakika 3:37.23, Timothy Cheruiyot wa Magereza (3:37.28) na afisa wa polisi Abel Kipsang (3:40.20) katika usanjari huo.

Celestine Biwot wa KDF (9:36.37), Diana Chepkemoi wa Nairobi (9:56.60) na Caren Chebet kutoka Magereza (10:01.64) walifuatana nafasi tatu za kwanza za 3,000m kuruka viunzi na maji. Bingwa wa Michezo ya Jumuiya ya Madola, Jackline Chepkoech, aliridhika na nafasi ya nne kwa dakika 10.04.98 kutoka orodha ya wakimbiaji 23.

Nafasi tatu za kwanza za 3,000m kuruka viunzi na maji kwa upande wa wanaume zilinyakuliwa na Simon Koech aliyeshinda pia mwaka 2022 na 2023. Koech kutoka KDF aliandikisha kasi bora ya dakika 8:22.99 akifuatiwa na Abraham Kibiwott wa Polisi (8:36.10) na bingwa wa Michezo ya Afrika 2019 Benjamin Kigen kutoka KDF (8:39.75).

Rebecca Mwangi wa Magereza akitumia dakika 15:39.78, Cynthia Chepkirui wa Polisi (15:40.83) na Faith Chebet wa South Rift (15:45.62) walifagia medali za 5,000m katika usanjari huo. South Rift ilitawala nafasi mbili za kwanza kwa upande wa wanaume kupitia kwa Gilbert Kiprotich (13:37.06) na Amos Kiprotich (13:37.58) nao George Manangoi wa KDF (13:43.03) na Alex Matata wa Magereza (13:50.91) wakafunga nne-bora, mtawalia.

Taji la wanaume la 10,000m lilinyakuliwa na Silas Senchura kutoka Polisi aliyeduwaza veterani Edwin Soi wa South Rift katika mita 10 za mwisho wakimaliza mizunguko hiyo 25 kwa dakika 28:26.17 na 28:29.19 mtawalia. Kelvin Rotich wa kanda ya Central Rift aliridhika na nafasi ya tatu kwa dakika 28:30.01 naye Daniel Simiu aliyepigiwa upatu sana kuwika akiridhika na nambari nne (28:30.89).

Idara ya Polisi ilifagia medali zote za kitengo cha wanawake katika kurusha tufe – hammer throw – kupitia kwa Roseline Rakamba (mtupo wa mita 55.64), Rebecca Kerubo (48.69m) na Nancy Kanini (48.06m). Nao wanajeshi Dominic Abunda (61.51m), Museveni Nyambasora (56.15m) na Denis Sakawa (53.17m) wakafanya vivyo hivyo upande wa wanaume.

Sarah Okumu, Belinda Oburu na Njau Ruguru kutoka KDF walinyakua dhahabu, fedha na shaba za kurusha tufe baada ya kuandikisha mitupo ya 15.34m, 15.15m na 14.56m mtawalia. George Malala na Benson Wachira kutoka KDF walifagia nafasi mbili za kwanza kurusha tufe upande wa wanaume wakiwa na mitupo ya 16.44m na 15.95m mtawalia. Peter Mwangi wa Magereza alifunga tatu-bora kwa 15.47m.

Faith Jepkemoi na Eucabeth Chepkemoi kutoka KDF walivuna medali ya dhahabu na fedha katika kuruka juu – high jump – mita 1.70 na 1.60 mtawalia. Moureen Wafula wa Magereza aliridhika na shaba (1.60m).

Asbel Kiprop wa KDF, Edwin Too wa Magereza na Abed Kiprotich kutoka Central Rift walifagia medali za kuruka juu baada ya kuandikisha matokeo ya 2.10m, 2.01m na 1.99m mtawalia.

Julius Yego wa Polisi akirusha mkuki . PICHA | CHRIS OMOLLO

Katika kuruka umbali – long jump – Faith Jepkemoi (6.60m) na Martha Nyabuto (5.90m) wa KDF na Idah Jepkorir wa Polisi (5.85m) walinyakua tatu-bora. Kevin Kemboi wa Polisi (7.73m), Too wa Magereza (7.62m) na Bismark Soi kutoka KDF (7.45m) wakafuatana katika usanjari huo katika kitengo cha wanaume.

Nyabuto pia alitwaa taji la kuruka utatu – triple jump – kwa mita 12.83 akifuatiwa na Jepkemoi (12.48m) na Jepkorir (12.16m). KDF pia ilitamba katika kuruka utatu upande wa wanaume kupitia Amos Mwendwa (16.14m) na Gilbert Pkemoi (16.13m) naye Mark Kiptoo kutoka NYS akawa nambari tatu (15.88m).

Mkazi wa Amerika, Irene Chepkemoi, na gunge Julius Yego walishindia Idara ya Polisi dhahabu ya kurusha mkuki – javelin – baada ya kuandikisha mtupo bora wa mita 57.88 na 79.27 mtawalia. Wawili hao wanashikilia rekodi ya kitaifa 60.31m na 92.72m mtawalia.

Katika kupokezana vijiti, kinadada kutoka KDF walitawala 4x100m kwa sekunde 45.57 wakifuatiwa na polisi (45.63) na magereza (45.75) mtawalia.

KDF ilitwaa dhahabu ya 4x100m ya wanaume kupitia kwa Meshack Babu, Justin Isaboke, Ekwam na Steve Onyango (sekunde 38.76). Ilifuatiwa na Idara ya Polisi kupitia kwa Richard Ogutu, Dennis Mwai, Ronald Koech na Omanyala (sekunde 38.78). Kisha Idara ya Magereza kupitia kwa Martin Juma, Hesbon Ochieng, Elkana Sabila na Kelvin Kipkorir (sekunde 40.33).

Polisi, KDF na Magereza zilitwaa nafasi tatu za kwanza katika 4x400m wanawake kwa dakika 3:27.22, 3:28.65 na 3:37.96 mtawalia. Maafisa wa polisi pia walitwaa dhahabu ya 4x400m wanaume wakifuatiwa na Magereza na KDF kwa dakika 3:00.99, 3:01.47 na 3:01.92 mtawalia.

Sylvia Cherono aliibuka malkia mpya wa kutembea haraka 20 kilomita baada ya kukata utepe kwa saa 1:43:34 mbele ya wanajeshi Caren Naliaka (1:46:26) na Naum Jepkirui (1:50.23). Mfalme wa zamani wa Afrika wa 20km, Samuel Gathimba kutoka Magereza, alinyakua taji katika fani yake kwa saa 1:25:37 akifuatiwa na wanajeshi Stephen Ndangili (1:27:33) na Albert Mwenda (1:29:58).