Dimba

Rising Starlets watua Dar kutesa Tanzania

Na TOTO AREGE February 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KIKOSI cha wachezaji 23 wa Rising Starlets kiliwasili Dar es Salaam, Tanzania mapema jana, kujiandaa kwa mechi ya marudiano ya raundi ya tatu ya kufuzu Kombe la Dunia la wachezaji wasiozidi umri wa miaka 20 dhidi ya Tanzanite Queens ya Tanzania.

Mechi hiyo itagaragazwa katika uwanja wa Azam Sport Complex Chamazi, Dar es Salaam kuanzia saa kumi jioni Jumamosi hii.

Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) lilitangaza jana kuwa mashabiki hawatatozwa ada ya kiingilio kwa mechi hii.

Kuelekea mechi hii, Starlets wanajivunia faida ya bao moja baada ya ushindi wa 1-0 katika mechi ya mkondo wa kwanza mnamo Jumamosi iliyopita katika uwanja wa Ulinzi Sports Complex jijini Nairobi.

Mshambuliaji Elizabeth Mideva alifunga bao hilo la pekee dakika ya 85 ya mchezo.

Kenya iko guu moja ndani ya raundi ya nne na ya mwisho, ikihitaji sare ya aina yoyote katika mechi ya marudiano ili kusonga mbele.

Kwa kuwa Tanzania watakauwa nyumbani mbele ya mashabiki wao, Starlets wanafaa kutumia nafasi zao vizuri za kufunga na waepuke kuruhusu bao, jambo ambalo kocha Jackline Juma, anafaa kulifanyia kazi baada ya kupoteza nafasi nyingi za wazi Jumamosi.

Mshindi wa jumla ya mabao atamenyana na mshindi kati ya Cameroon na Botswana mwezi Mei katika raundi ya mwisho.

Cameroon iliikomoa Botswana 5-0 katika mechi ya mkondo wa kwanza mjini Yaounde, Cameroon, Jumamosi. Mechi ya marudiano itachezwa Francistown, Botswana, Jumamosi hii.

Kenya na Tanzania zinatafuta tiketi ya kufuzu Kombe la Dunia kwa mara ya kwanza katika kitengo hiki (U20).

Dimba hilo litaandaliwa nchini Poland kuanzia Septemba 5 hadi 17 mwaka huu.