Dimba

Ruto aongoza mashabiki wa Arsenal ulimwenguni kuipongeza timu kwa ushindi

Na CECIL ODONGO May 20th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

‘ERLING Halaand alipofunga dakika za lala salama za muda wa ziada mwishoni mwa kipindi cha pili, mwili ulizizima. Nilijua Manchester City wangepata bao jingine lakini kipenga cha mwisho kilipopulizwa, nilipiga nduru.”

Haya ni maneno ya Mhariri Msanifishaji wa Taifa Leo Steven Musamali ambaye hangeweza kuzuia furaha iliyomvaa baada ya Arsenal kushinda ubingwa wa Ligi Kuu Uingereza (EPL) mnamo Jumanne usiku.

Hili lilikuwa taji la kwanza la Arsenal baada ya ukame wa miaka 22.

Akitabasamu na kucheka na kila mtu, Musamali alikuwa kati ya umayamaya wa mashabiki wa Arsenal kote Kenya na mataifa ya nje ambao walikuwa wamesisimuliwa na ushindi huo adimu.

Manchester City walifunga bao dakika za jioni na kupata sare ya 1-1 dhidi ya Bournemouth ugani Vitality. Matokeo hayo yalizamisha juhudi zao za kushinda ubingwa wa EPL ikiwa imesalia mechi moja msimu uishe.

Arsenal watapokezwa kombe mnamo Jumapili uwanja wa Selhurst Park baada ya kucheza mechi yao ya mwisho dhidi ya Crystal Palace.

Kote nchini, sherehe zilianza mara moja. Mitandao ya kijamii ilijaa jumbe za pongezi, utani na mashabiki ambao walijaa hisia tele.

Baadhi hata walichukua muda wao kuwadhihaki mashabiki wa Manchester United ambao walishinda ubingwa wa EPL miaka 14 iliyopita.

“Video ya wachezaji wa Arsenal wakitazama na kusherehekea ilinipeleka nje ya dunia hii. Nimelia, na sijui niseme nini kwa sababu misimu mitatu iliyopita tumekuwa tukimaliza nambari mbili na kukaribia kutwaa taji,” akaandika Ignatious Realtor katika ukumbi wa WhatsApp inayofahamika kama Sports ambayo ina mashabiki wa soka wa klabu mbalimbali.

Hata Rais William Ruto alihepa changamoto ambazo zimekuwa zikizonga nchi kutokana na kupanda kwa bei ya mafuta na kupongeza Arsenal.

“Nimefuatilia Arsenal nyakati ngumu na furaha na safari yao ya kurejea katika ufanisi wa soka ni ya kuigwa kiasi kwamba wameshinda EPL. Timu imeshinda, juhudi na nia zimezaa matunda. Hongera sana Arsenal,” akasema Rais Ruto ambaye yupo kwenye ziara ya siku mbili kule Kazakhstan.

Arsenal pia ilipongezwa na Rais wa Rwanda Paul Kagame ambaye taifa lake linashirikiana na timu hiyo kupitia nembo ya ‘Visit Rwanda’ kwenye jezi zao.

“Manchester United hawajashinda EPL kwa miaka 13. Hiyo timu haina umakini kuhusu mambo ya mpira,” akaandika Alinur Mohamed kwenye ukurasa wake Facebook akiwadhihaki mashabiki wa mahasimu hao wa Arsenal.

Sherehe za mashabiki hata hivyo ziliingiwa na ukiwa kiasi, wengi wakimkumbuka marehemu Waziri Mkuu Raila Odinga ambaye aliaga dunia pamoja na wengine ambao pia walitangulia mbele za haki.

Kiongozi huyo wa ODM ambaye aliaga dunia mnamo Oktoba mwaka jana, alikuwa shabiki wa Arsenal na alikuwa akitembelea uga wa Emirates mara kwa mara kushuhudia mechi za timu hiyo.

“Arsenal imeishindia, Baba Raila Amollo Odinga EPL” akaandika Luyali Alumasa kwenye X akiambatanisha na ishara ya kulia.

Mashabiki wa Arsenal sasa wanapanga kuteka miji mbalimbali Jumapili hii ambapo timu hiyo itakuwa ikikabidhiwa rasmi taji lao.

Kundi la Arsenal Fanatics nalo linapanga kuteka jiji la Nairobi ambapo watajumuika pamoja kutazama mechi dhidi ya Crystal Palace Jumapili.

Hakika miaka 20 ya kusuburi hatimaye imezaa matunda.