Ushindi dhidi ya Spurs umetuondolea aibu ya Wolves, Arteta akiri
MIKEL Arteta alikiri ubora wa kikosi chake katika ushindi wa 4-1 dhidi ya Tottenham Spurs Jumapili usiku Ugani Tottenham Spurs, baada ya “aibu” ya sare ya 2-2 dhidi ya Wolves wiki jana katika mechi ya Ligi Kuu ya Uingereza (EPL).
Eberechi Eze (32 na 61) na Viktor Gyökeres (47 na 94) wote walifunga mara mbili. Kolo Muani alifungia wenyeji bao la kufutia machozi dakika ya 34.
The Gunners sasa wameshinda mara 63 katika mechi 198 za debi ya London Kaskazini na huu ulikuwa ushindi wa tano mfululizo dhidi ya Spurs rekodi yao bora tangu 1989.
Uimara wa Gunners umekuwa ukitiliwa shaka mara kwa mara msimu huu na ukosoaji huo uliongezeka baada ya kutoka sare dhidi ya wavuta mkia Wolves.
“Nahisi tulionyesha ubora wetu,” Arteta alisema baada ya mechi. “Lakini basi lazima uonyeshe tena na tena na tena kwa sababu, ikiwa unapaswa kuchambua tu jinsi unavyohisi baada ya kila mchezo, hili linakuja na hisia mseto.”
Aliongezea akisema, “Baada ya kile kilichotokea dhidi ya Wolves na jinsi tulipoteza alama mbili katika dakika ya mwisho ya mchezo, ilikuwa ngumu. Lakini huo ndio uzuri wa mchezo huu. Hakuna kuangalia nyuma ila utaangalia nyuma na kuapa halitokei tena.”
Kocha wa muda wa Spurs Igor Tudor ambaye alichukua mikoba ya Thomas Frank ambaye alitimuliwa wiki jana alisema, “Nina huzuni hatukupambana vya kutosha. Arsenal walikuwa bora zaidi. Kulikuwa na pengo kubwa kati ya timu hizi mbili.”
Baada ya ushindi huo, Arsenal walifungua mwanya wa alama tano kileleni mwa jedwali wakiwa na alama 61. Wapinzani wao wa karibu Machester City wameshikilia nafasi ya pili na alama 56 wakiwa na mechi moja kibindoni. Spurs nao waliendelea kusalia nafasi ya 16 na alama 29.
Katika mechi zingine Jumapili, Liverpool walivuna alama zote dakika za lala salama kipindi cha pili kutoka na bao la Mac Allister dhidi ya Forest Ugani The City Ground. Sunderland walinyoroshwa 3-1 na Fulham nao Crystal Palace wakaponyoka na ushindi wa 1-0 dhidi ya Wolves.