Walioshinda medali Riadha za Dunia walia ahadi hewa za serikali
WASHINDI wa medali wa Timu ya Kenya katika Riadha za Dunia za Mbio za Milimani (WMTRC) za 2025 bado wako mbioni, lakini si kupanda mlima tena, bali kwa kuishiwa subira kwani hawajatunukiwa zawadi zao.
Miezi kadhaa baada ya kupeperusha vilivyo bendera ya Kenya katika mashindano hayo ya dunia, wanariadha hao bado hawajalipwa zawadi za fedha zilizoahidiwa na serikali kwa washindi wa medali katika mashindano makubwa ya kimataifa.
Timu hiyo inadai jumla ya Sh1,645,287 (Euro 10,750) kupitia mradi wa kitaifa wa zawadi, kwa mafanikio yao katika riadha za WMTRC zilizofanyika Canfranc, Uhispania, mnamo Septemba 25-28.
Philemon Kiriago aliiongoza Kenya kwa ushindi wa dhahabu katika kitengo cha Mountain Classic cha wanaume, akitumia saa 1:02:30, mbele ya Martin Kiprotich wa Uganda (1:03:14) huku Paul Machoka akiridhika na shaba kwa 1:03:25.
Ushindi huo ulikuwa ishara ya ubabe wa Kenya unaokuwa katika mbio za milimani.
Richard Atuya alinyakua fedha katika mbio kali za Vertical Uphill kwa dakika 39:04, akimfuata bingwa Remi Bonnet wa Uswisi (37:50), huku Patrick Kipngeno akichukua shaba kwa 39:20, akithibitisha kina cha Kenya katika mbio za miinuko mikali.
Kwa upande wa wanawake, Ruth Gitonga alipata fedha katika Mountain Classic kwa 1:12:54, nyuma ya Nina Engelhard wa Ujerumani (1:11:00) na mbele ya Oria Liaci wa Uswisi (1:13:15).
Joyce Njeru pia alichangia pakubwa Kenya kutwaa mataji ya Timu ya Mountain Classic kwa wanaume na wanawake, ushindi wa kihistoria ulioiweka Kenya kileleni kwa ubora wa timu.
Hata hivyo, nyumbani shangwe zimegeuka kuwa masikitiko.
“Bado hatujalipwa zawadi zetu za fedha kwa mafanikio ya Uhispania. Tunaomba serikali itimize ahadi yake,” alisema Kiriago.
Kwa wanariadha wa mbio za milimani wa Kenya, medali tayari ni historia.
Kinachosubiriwa sasa ni utekelezaji wa ahadi, si kwa makofi, bali kwa vitendo.