• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 10:15 PM
Afokea pasta kwa kumkataza kuoa kidosho

Afokea pasta kwa kumkataza kuoa kidosho

NA JOHN MUSYOKI

MATENDENI, EMBU

MUUMINI wa kanisa moja hapa alimkemea pasta kwa kukataa kumsaidia kutafuta kidosho mrembo wa kuoa katika kanisa lake.

Duru zinasema jamaa alikuwa amekosa kuoa na akaamua kuomba usaidizi kutoka kwa pasta. Hata hivyo baada ya kumrai pasta amtafutie demu kanisani, mchungaji alikataa na kumkera sana jamaa huyo.

Juzi jamaa alisikika akidai pasta alikuwa na maringo sana. “Sijui pasta huyu wetu ni wa sampuli gani! Nilimwambia kitambo anitafutie demu mrembo kanisani nimuoe lakini amenipuuza tu,” jamaa alisema kwa hasira.

Inasemekana watu walipigwa na mshangao mkubwa na kutaka jamaa huyo awafafanulie ni kwa nini alimtaka pasta amtafutie mwanamke wa kuoa kanisani.

Aliwajibu; “Kabla sijaokoka, pasta aliniambia nikikubali kutubu na kuacha dhambi atanitafutia msichana mrembo kanisani nimuoe. Sasa nimesubiri kwa muda mrefu na sijaona akishughulika. Wasichana wengi wameolewa nikiwa hapa tu na wamepungua sana. Nitasubiri mpaka lini?” jamaa alisema.

Hata hivyo waumini walipomdadisi pasta alidai kwamba jamaa huyo hakuwa amekomaa kuwa na mke. Alisema kuoa kunahitaji mtu kukomaa kiroho na hawezi kupendekeza mwanadada kuolewa na limbukeni katika imani.

“Bado kijana hajakomaa na itabidi asubiri hadi pale Mungu atakapojibu maombi yake,” pasta alisema.

Kulingana na mdokezi, pasta alishuku jamaa alikubali kuokoka ili kupata mke kanisani pekee.

Jamaa aliposikia hivyo alichemka zaidi na kuapa kugura kanisa la pasta huyo kwa kutotimiza ahadi yake.

Waumini walishuku huenda maneno ya pasta yalikuwa ya kweli. Hata hivyo haikujulikana kilichojiri baada ya kioja hicho.

You can share this post!

Uhamisho wa walimu walemaza masomo

Ngunjiri asalimisha bunduki yake kwa polisi

adminleo