Dondoo

Aliyeibia mamake aomba asipitishwe karibu na makazi ya demu wake akipelekwa kwa chifu

Na BENSON MATHEKA February 10th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KALAMENI aliyekamatwa na mzee wa nyumba kumi na wanakijiji kwa kuiba pesa za mama yake alizua kicheko alipoomba asipitishwe karibu na boma ya demu aliyekuwa akimchumbia katika safari ya kuelekea kwa chifu.

Jamaa huyo alimwibia mama yake pesa za chama cha wanawake na kwenda kuponda raha mtaani.

Mama yake alimshtaki kwa mzee wa nyumba kumi ili atafutwe na msako ukaanza mara moja.

Baada ya siku kadhaa jamaa alikamatwa na akaanza kusihi mzee wa nyumba kumi na wanakijiji asikosewe heshima zaidi kwa kupitishwa karibu na boma ya mtu wake.

“Kama tutatembea kwa miguu mkiwa mmenifunga kamba mikononi kwa njia hii, naomba tusipite njia ya boma la wakwe wangu watarajiwa. Heri wasikie habari kunihusu badala ya kuniona nikiwa nimefungwa kwa kamba mikononi,” jamaa alilalamika na watu wakaangua vicheko tu.