• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 11:13 AM
Demu afichua mumewe amemnyima asali kwa miaka 4

Demu afichua mumewe amemnyima asali kwa miaka 4

Na TOBBIE WEKESA

WANGURU, KIRINYAGA

Kipusa mmoja kutoka hapa aliwashangaza wengi alipodai ndoa yake haina ladha. Mwanadada huyo alidai kuwa tangu aolewe miaka minne iliyopita mumewe hajawahi kumgusa.

Inadaiwa aliitisha kikao cha dharura na wazee wa kanisa baada ya kugundua kwamba mumewe hakuwa akichangamkia tendo la ndoa.

“Miaka minne sasa imepita lakini hajawahi kunigusa kamwe. Hata kunikaribia kitandani hataki,” mrembo alidai.

Wazee wa kanisa walitulia huku kidosho akiendelea kutoa kauli zake.

“Tulipokuwa tukichumbiana aliniambia tusile tunda kwanza hadi tutakapooana. Sasa tumeoana na bado ananiambia ni mapema sana kula tunda,” kipusa aliendelea kusema.

Wazee wa kanisa walibaki kuangaliana huku wengine wakiangalia chini.

“Mimi nina hisia. Nitangoja hadi lini ilhali natamani raha ya ndoa?” kipusa aliwauliza wazee wa kanisa.

Waliohudhuria kikao hiki walibaki vinywa wazi. “Tulipoenda fungate, nilishangaa sana bwanangu aliponiambia hayuko tayari kuonja asali,” kipusa alisema huku akiketi.

Wazee wa kanisa walimrai polo ajitetee naye akadai mrembo anampeleka mbio.

“Huyu mwanamke aache mbio. Kila mechi huwa na maandalizi. Ningali najiandaa. Makombora yaja,” polo alidai huku vicheko vikishamiri. Duru zinasema kipusa aliinuka na kumshutumu jamaa kwa kutosema ukweli.

“Unajiandaa hadi lini? Ni mechi gani hii unayodai unajiandaa. Wewe sema ukweli,” kidosho alifoka.

Penyenye zinasema wazee wa kanisa waliwarai wanandoa hao kuwa na subira huku wakitafuta suluhisho. Hata hivyo mwanadada alisema hangesubiri na akaapa kumuacha jamaa iwapo wazee hawangesuluhisha suala hilo.

“Subira hadi lini. Mimi naomba kumpa huyu jamaa talaka. Hata kitandani analala na nguo. Sijui anaficha nini,” kipusa alitishia.

 

You can share this post!

Jumla ya watu 563 wamekufa kutokana na virusi vya Corona

Zawadi ya bathdei ya Ronaldo ni gari la Sh14.9 milioni

adminleo