Dondoo

Jombi ahamisha makazi ufukweni ili kuhepa kero za mke nyumbani

Na KALUME KAZUNGU March 24th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

AMU KISIWANI, LAMU

JOMBI mmoja kisiwani Lamu amewaacha wengi vinywa wazi baada ya kuamua kuhamisha makazi yake hadi karibu na bahari, akisema huko ndiko amepata utulivu wa kweli.

Jamaa huyo amejitengenezea maskani ndogo karibu na ufukwe wa Bahari Hindi ambako hulala usiku
Alipoulizwa kwa nini alichukua hatua hiyo ya ajabu, jombi huyo alisema ni afadhali kuvumilia baridi kali, unyevunyevu na chumvi ya bahari kuliko kusikiliza kelele za kila mara kutoka mkewe.

Kwa mujibu wake, mkewe amekuwa mgomvi na mkali kiasi cha kumkosesha amani nyumbani.

Anasema alihofia hata afya yake ya akili kuathirika iwapo angeendelea kuishi katika mazingira hayo.

Jombi huyo anasema mawimbi ya bahari na upepo mwanana humtuliza sana akili.

“Nitaendelea kulala hapa. Hapa kuna utulivu na amani. Mke wangu abaki na kelele zake huko nyumbani,” alisema kwa msisitizo.