Mganga afanya buda kuleta mpango wa kando nyumbani
MIDODONI, Gongoni
KILIKUWA kioja cha mwaka kijijini hapa buda aliyekuwa akimtesa mkewe kwa kulalalala na mipango ya kando alipojipata amemleta mmoja wa vimada wake nyumbani bila kufahamu.
Mzee huyo ambaye ameishi kwa ndoa kwa zaidi ya miaka 20 na kujaliwa watoto watano, amekuwa akimwacha mkewe na kilio hasa tangu alipofanikiwa kununua gari.
Wanaomfahamu wanasema amekuwa akilitumia sana gari lake kubeba mipango wake wa kando na kuenda nao gesti kupiga sherehe.
Kila alipoulizwa na mkewe, buda amekuwa akitoa kucha na kumfokea kwa ukali. Ni hali iliyomchosha mkewe akatafuta huduma za mganga wa kumzindika mume huyo.
Baada ya wiki moja hivi, jamaa alianza kuchanganyikiwa hasa kila anapojaribu kuendeleza tabia zake.
Siku hiyo, alifika mjini kwa shughuli za kikazi na bila kupoteza muda alijitwalia kipusa kuenda naye gesti.
Safari hii alijikuta akiendesha gari kwa kasi kuelekea kwao mashambani na kimada badala ya gesti.
Demu alipomuuliza wanakokuwa wakienda alimwarifu kuwa ametafuta gesti murwa iliyoko sehemu fiche, nje ya mji.
Kufumba na kufumbua, jamaa alijipata akisimamisha gari mbele ya nyumba yake na kutoka nje akiwa amemshikilia mrembo huyo.
Alibisha mlango wa nyumba yake akidhani anaingia gesti.
Macho yake yalifunguka punde alipomwona mkewe wa ndoa akimfungulia mlango kuwakaribisha ndani na kimada wake nusura aanguke.