• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 10:50 AM
Pasta adinda kuombea polo aliyekataa kuoa bintiye

Pasta adinda kuombea polo aliyekataa kuoa bintiye

Na John Musyoki

OTHAYA, Nyeri

Pasta wa kanisa moja eneo hili, alishangaza waumini alipodinda kumuombea jamaa aliyekataa kuoa binti yake.

Penyenye zinasema jamaa alikuwa akimchumbia binti wa pasta huyo lakini kwa sababu ambazo hazikueleweka alikataa kumuoa na akafunga ndoa na mwanadada mwingine wa kijiji chao.

Siku ya kioja jamaa alikuwa ameugua na waumini wa kanisa wakamuomba pasta amtembelee nyumbani kwake akamuombee.

Pasta kusikia hivyo, alichemka na kuanza kulalamika akidai jamaa huyo alikuwa amemkosea sana.

“Maombi yana gharama yake. Nilikuwa na matumaini makubwa kwa jamaa huyo kwamba angemuoa binti yangu ila hilo halikufanyika. Jamaa huyo aliharibia binti yangu muda na simpendi. Kama mnamjali nendeni mkamuombee,” pasta aliwaambia waumini wake.

Waumini wa pasta huyo walishangaa na kumgombeza pasta huyo kwa kukataa kwenda kumwombea jamaa.

“Wewe ni pasta wa sampuli gani kama una wivu na roho ngumu kama chuma. Jamaa huyo alikuwa na haki ya kuoa msichana aliyempenda. Kumbuka wahenga walisema kuwa, kuchumbia sio kuoa,” mwanadada mmoja alimwambia pasta.

Hata hivyo waumini wa pasta huyo waliamini na kufunga safari ya kwenda kumwombea jamaa. Inasemekana baada ya siku chache, jamaa alipata nafuu na kurejelea hali yake ya kawaida.

Aliposikia pasta alikataa kwenda kumuombea, jamaa alisikitika sana na kusema pasta alikuwa akimlazimisha aoe binti yake.

“Nasikitika pasta anaweza kuwa na machungu kwa sababu nilikataa aliponilazimisha kuoa binti yake. Naona jambo la muhimu kufanya ni kuhama kanisa lake ili awe na amani,” jamaa alisema.

Haikujukana ikiwa jamaa huyo alihama kanisa hilo au la.

You can share this post!

Coronavirus sasa yafika Afrika, Algeria yatangulia

Bunge laidhinisha Mutahi Kagwe na Betty Maina kuwa mawaziri

adminleo