• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 5:55 AM
Polo mtafuna yaya afumaniwa na mke wakati wa corona

Polo mtafuna yaya afumaniwa na mke wakati wa corona

KAPKATET, KERICHO

NA NICHOLAS CHERUIYOT

ILIBIDI polo wa hapa akubali kwa haraka kufanya kazi za jikoni ili kuokoa ndoa yake baada ya kufumaniwa akinyemelea yaya.

Tamaa ya jamaa ilivuka mipaka akawa anawatafuna yaya ambao mkewe alikuwa akiajiri.

Semasema za mtaa zaeleza kuwa, tangu kuzuka kwa corona, jamaa alipewa likizo ndefu na kampuni anayoifanyia kazi lakini mkewe akawa bado anaendelea kufanya kazi.

“Mke akienda kazi jamaa alibaki nyumbani pamoja na mtoto wao na meidi. Mkewe alihofia kuwa mumewe alikuwa akimnyemelea meidi ndipo akaanza kuwa mpekuzi wa mambo sana,” mdaku akaarifu.

Juzi mkewe alitoka kazini mapema na kumfumania mume akimpapasa yaya jikoni. Wawili hawa walitengana ghafla nusura wamwage chakula kilichokuwa motoni.

Yaya huyo alipigwa kalamu mara moja na mwingine akachukua nafasi yake siku iliyofuata.

“Nimemtafuta asiye na sura wala mwili wa kuteka hisia za mume wangu lakini bado niko macho,” mrembo alinukuliwa akiambia mashogake.

Mambo yalizidi unga hata zaidi alipofika nyumbani na kuripotiwa na yaya kuwa mumewe alimtongoza mchana kutwa.

“Hakuniacha nifanye kazi leo. Alinifuata akiniambia maneno ya kimahaba lakini nilimpuuza na kudinda kumtimizia tamaa yake,” kidosho alimshtaki jombi.

Mkewe alivunjika moyo sana na baada ya kuwaza na kuwazua, akaamua kuwaita jamaa za mumewe kuokoa jahazi lisizame.

“Iliamuliwa kikaoni kuwa yaya afutwe na mzigo wa kazi za jikoni utwikwe jombi naye akakubali kufanya hivyo ili mke asimtoroke,” mdaku akasema.

Kwa sasa jamaa huonekana akijikaza vilivyo kwa kazi za upishi, kutunza mtoto, kupiga deki na kuosha vyombo kila siku.

You can share this post!

Trump aashiria kutong’atuka akishindwa uchaguzini ujao

Vimada wafyonza jasho la paparazzi

adminleo