Michezo

Duru mpya ya Kakamega Sevens yaongezwa katika raga za kitaifa

March 8th, 2019 2 min read

Na GEOFFREY ANENE

DURU mpya ya Kakamega Sevens imejumuishwa kwenye Raga za Kitaifa za wachezaji saba kila upande, ambazo ratiba yake ya mwaka 2019 imetangazwa Ijumaa.

Kakamega Sevens, ambayo inaingia katika mashindano haya yanayofanyika kila mwaka tangu mwaka 1999, imejaza nafasi ya duru ya Sepetuka Sevens, ambayo imeondolewa.

Duru ya Kakamega itakuwa ya kwanza kuandalia. Timu zitashindania taji mnamo Julai 20-21, wenyeji wakiwa timu ya Western Bulls, ambayo ilitemwa kutoka Ligi Kuu misimu miwili iliyopita, na mabingwa wa Kenya mwaka 2016 Kabras Sugar. Bulls na Kabras zinatoka katika kaunti ya Kakamega.

Mwaka 2017, klabu ya Homeboyz iliomba kuandaa duru moja kwa kipindi cha miaka miaka. Homeboyz ndio ilikuwa mwenyeji wa Sepetuka Sevens mwaka 2017 na 2018 mjini Eldoret. Ombi la pamoja kutoka kwa Kabras na Bulls litashuhudia Kakamega ikiwa mwenyeji wa Kakamega Sevens mwaka 2019 na 2020.

Baada ya kuzuru Kakamega, timu zitaelekea jijini Nairobi kwa duru ya pili ya George Mwangi Kabeberi Sevens uwanjani RFUEA Grounds. Duru hii ambayo mwenyeji wake ni klabu ya Mwamba, inarejea jijini baada ya kuandaliwa mjini Machakos mwaka 2018. Mwaka huu itafanyika Julai 27-29. Raga hii kisha itachukua likizo Agosti 3-4 kabla ya kuendelea Agosti 10-11 ambapo mji wa Kisumu utaandaa Dala Sevens uwanjani Mamboleo Showground ASK.

Duru ya Prinsloo itafuatia mnamo Agosti 17-18 mjini Nakuru kabla ya Kenya Harlequins kuandaa Christie Sevens uwanjani RFUEA Grounds na kisha duru ya Driftwood Sevens kufunga mwaka mnamo Septemba 7-8 mjini Mombasa.

Homeboyz ndio mabingwa watetezi. ‘Madeejay’ hawa walishinda Prinsloo, Kabeberi, Sepetuka na Christie. Mwamba ilimaliza katika nafasi ya pili baada ya kufika fainali tatu na kutwaa taji la Dala Sevens.

Ratiba ya mwaka 2019

Julai 20-21: Kakamega Sevens, Bull Ring Kakamega

Julai 27-28: Kabeberi Sevens, RFUEA Grounds

Agosti 3-4: Mapumziko

Agosti 10-11: Dala Sevens, Mamboleo Showground ASK

Agosti 17-18: Prinsloo Sevens, Nakuru Athletics Club

Agosti 24-25: Mapumziko

Agosti 31 na Septemba 1: Christie Sevens, RFUEA Grounds

Septemba 7-8: Driftwood Sevens, Mombasa Sports Club

Washindi wa raga za kitaifa

1999 Impala Saracens

2000 Impala Saracens

2001 Impala Saracens

2002 Ulinzi

2003 Ulinzi

2004 Impala Saracens

2005 Kenya Harlequin

2006 Kenya Harlequin

2007 Mwamba

2008 Mwamba

2009 Strathmore Leos

2010 Mwamba

2011 Mwamba

2012 Kenya Harlequin

2013 KCB

2014 KCB

2015 Nakuru

2016 Homeboyz

2017 Kabras Sugar

2019 ?