Habari Mseto

Mzozo katika baa ulivyosukuma baba, wanawe 3 na mkwe jela miaka 100

Na JOSEPH WANGUI June 9th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

MWANAMUME mwenye umri wa miaka 61, wanawe watatu na mkwe wao wamepoteza rufaa waliyowasilisha kupinga kifungo cha jumla ya miaka 100 jela, baada ya kupatikana na hatia ya kumshambulia jirani yao kufuatia ugomvi uliotokea baa.

Kifungo cha watano hao mnamo Aprili 2024 kilitokana na kukwama kwa juhudi za upatanisho zilizofanywa na chifu wa kijiji chao.

Bw John Ritho Kiboi na wanawe walihukumiwa kwa kosa la kumshambulia Bw John Gichuki.

Wakati wa juhudi za upatanisho, familia hiyo ilikubali kumlipa Bw Gichuki gharama ya matibabu iliyofikia Sh800,000. Hata hivyo, walikataa kulipa na wakaamua kushughulikia suala hilo mahakamani.

Mkasa huu ulianza baada ya mzozo kati ya Bw Kiboi na Bw Gichuki ndani ya baa iliyopo katika kituo cha biashara cha Ganyuthe, eneo la Kieni Magharibi, kaunti ya Nyeri, usiku wa Novemba 17, 2019.

Wawili hao walikuwa wakibugia vileo, kila mmoja akiwa ameketi meza tofauti. Bw Gichuki alikuwa na mkewe, huku Bw Kiboi akiwa na wateja wengine, akiwemo mkwe wake Evans Waititu.

Chanzo cha mzozo huo kilisemekana kuwa maneno ya kejeli yaliyotamkwa na kundi la Bw Kiboi, ambapo Bw Gichuki alisikiliza mazungumzo yao yaliyokuwa yakimdhalilisha yeye na familia yake kwa kuwaita watu wa kiburi. Baada ya muda, mke wa Bw Gichuki aliondoka baa hiyo.

Baadaye usiku, Bw Gichuki alivamiwa akiwa njiani kuelekea nyumbani na watu watano wanaoaminika kuwa ni Bw Kiboi, wanawe watatu – John Ritho, Paul Kiboi, na Kenneth Wachira – pamoja na mkwe wake Waititu. Walimsababishia majeraha mabaya yaliyohatarisha maisha yake.

Ingawa shambulio hilo lilifanyika gizani bila shahidi wa moja kwa moja, Bw Gichuki alisema aliweza kuwatambua waliomshambulia, na maelezo yake yaliaminiwa na polisi pamoja na mahakama.

Wakili wao, Dkt Adrian Kamotho, alidai kuwa vipengele muhimu vya kosa hilo havikuthibitishwa pasipo shaka yoyote ya msingi, hasa kutokana na ukosefu wa kuwatambua kikamilifu washukiwa waliodaiwa kumshambulia mlalamikaji.

“Mahakama ilikosea kwa kutegemea ushahidi bila kuzingatia hali ya mwanga na muda ambao tukio linadaiwa kufanyika, hali iliyofanya iwe vigumu kwa shahidi kufanya utambuzi wa maana. Kwa hivyo, walioshtakiwa walipata hukumu isiyo ya haki,” alisema Dkt Kamotho.