Maaskofu walaani mauaji ya makasisi
KANISA Katoliki limelaani vikali mauaji ya hivi majuzi ya mapadri wake wawili, likitoa wito kwa serikali kuharakisha uchunguzi.
Katika taarifa iliyotolewa na Baraza la Maaskofu wa Kanisa Katoliki Kenya (KCCB) kupitia Idara ya Haki na Amani ya Kanisa Katoliki, Kanisa hilo limeeleza hasira na huzuni kubwa kufuatia kile linachotaja kuwa ni mauaji ya kulengwa.
“Tumesikitishwa sana na vifo vya ghafla vya mapadri wawili wa Kanisa Katoliki kwa muda mfupi,” ilisema taarifa ya maaskofu.
“Tunataka uchunguzi wa kina kuhusu vifo hivi ili kufichua mazingira na nia halisi, na kuhakikisha usalama wa mapadri wetu na Wakenya wote kwa ujumla.”
Padri John Maina, aliyepatikana akiwa hajitambui kando ya barabara ya Nyeri–Nyahururu, alifariki dunia alipokuwa akipokea matibabu hospitalini. Uchunguzi wa awali ulionyesha kuwa huenda padri huyo alitekwa kwa nguvu na kuteswa, kwani mwili wake ulionyesha dalili za kunyweshwa sumu au dawa hatari kwa lazima.
Katika taarifa yao, viongozi wa Kanisa Katoliki walithibitisha wasiwasi huu, wakisema kuna uwezekano mkubwa kuwa Padri Maina alikuwa mwathirika wa njama ya uhalifu.
Katika tukio tofauti na la kusikitisha zaidi, Padri Alois Bett, aliyekuwa akihudumu katika Jimbo Katoliki la Eldoret, alipigwa risasi na kuuawa na watu wasiojulikana katika eneo la Tot, Bonde la Kerio, Kaunti ya Elgeyo Marakwet. Ripoti zinaonyesha kuwa alikuwa akirejea katika kituo chake cha kazi baada ya kuongoza ibada kijijini.
Kwa mujibu wa walioshuhuda, watu hao walimpiga risasi mara kadhaa muda mfupi baada ya kumaliza misa ya Jumuiya Ndogo ya Kikristo katika kijiji cha Kakbiken.
Wakizungumzia kifo cha Padri Bett, Maaskofu wa Kanisa Katoliki walikitaja kama “mauaji ya kikatili”, huku wakieleza hofu yao kuhusu hali ya usalama katika maeneo yanayokumbwa na visa vya mara kwa mara vya mashambulizi.
Maaaskofu pia walisisitiza umuhimu mkubwa wa mapadri katika jamii, wakisema jukumu lao ni zaidi ya huduma za kiroho tu.
Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) imethibitisha kuwa uchunguzi unaendelea kuhusu kifo cha Padri Maina, ambaye alifariki dunia siku chache baada ya kuwa mwenyeji wa aliyekuwa Naibu Rais, Rigathi Gachagua wakati wa maadhimisho ya miaka 25 ya Parokia ya Igwamiti.