Korti yakataa kuwarudisha kazini wafanyakazi wa Gachagua
Mahakama ya Uajiri na Mahusiano ya Kazi jijini Nairobi imetupilia mbali kesi iliyopinga kufutwa kazi kwa wafanyakazi waliokuwa wakihudumu katika afisi ya Naibu Rais wa zamani Rigathi Gachagua, kufuatia kuondolewa kwake mamlakani Oktoba 2024.
Jaji Hellen Wasilwa alisema serikali haikuvunja haki za wafanyakazi waliodaiwa kufutwa kwa misingi ya kisiasa, akisisitiza kuwa waliokuwa wakifanya kazi kwa mkataba hawakuwa na haki ya kuendelea kuhudumu baada ya mkubwa wao kuondolewa mamlakani.
Wakili wa Nairobi Suyianka Lempaa, kwa ushirikiano na shirika la African Centre for Peace and Human Rights, walikuwa wamewasilisha ombi mahakamani wakidai kuwa hatua hiyo ilikuwa njama ya kuingiza siasa katika utumishi wa umma. Walisema kuwa kuwatimua wafanyakazi kwa sababu Gachagua alikosana na Rais ni sawa na kusema kuwa nao pia waliondolewa kwa mchakato usiotambuliwa na sheria.
“Watumishi wa umma hawapaswi kuwa nyasi zinazolaliwa wakati ndovu wawili wanapigana,” alisema wakili Lempaa mbele ya mahakama.
Aidha, alihoji kuwa kazi ya watumishi wa umma haifai kutegemea nani yuko mamlakani, kwani majukumu yao ni kwa manufaa ya wananchi wote bila kujali siasa.
Licha ya hoja hizo, Jaji Wasilwa alikubaliana na msimamo wa Tume ya Huduma za Umma (PSC) pamoja na Mwanasheria Mkuu kwamba wafanyakazi waliokuwa wameajiriwa kwa mkataba walipaswa kuondoka mara moja baada ya Gachagua kuondolewa ofisini.
“Itabainika wazi kuwa maafisa hao 61 walikuwa wameajiriwa kwa mkataba wa ndani ulioambatana na kipindi cha utawala wa Naibu Rais Rigathi Gachagua. Kwa kuwa aliondolewa mamlakani, mikataba yao ilikatika mara moja,” alisema Jaji Wasilwa.
Jaji aliongeza kuwa mikataba ya ajira iliyowasilishwa mahakamani haikuwa na ushahidi wa kutosha kuonyesha kuwa wafanyakazi hao walifutwa kwa njia isiyo halali.
“Walikubali kwa mkataba kuhudumu kwa muda wa Gachagua, na hawawezi sasa kudai vinginevyo. Sioni ukiukaji wowote wa kikatiba dhidi yao. Hivyo basi, ombi lao halina msingi na linatupiliwa mbali,” aliamua.
Wakili Lempaa alikuwa amepinga hatua ya serikali kuwatuma likizo ya lazima wafanyakazi hao bila kufuata utaratibu wa kisheria, akisema hatua hiyo ni dhuluma na unyanyasaji.
“Watumishi wa umma ni wa serikali, si wa mwanasiasa yeyote. Wanastahili kutekeleza majukumu yao bila kuonekana kuwa upande wowote wa kisiasa,” alisema Lempaa.
Tume ya Huduma ya Umma kupitia kwa Afisa Mkuu Mtendaji wake Paul Famba, ilieleza kuwa waliokuwa wameajiriwa kwa kandarasi walipaswa kuondoka kazini mara moja baada ya Gachagua kuondolewa. Hata hivyo, wafanyakazi waliokuwa katika nafasi za kudumu walihitajika kurejea kazini.
Famba alisema, “Mikataba ya walioajiriwa kwa kandarasi ilisitishwa rasmi mnamo Oktoba 17, 2024, siku aliyoondolewa Gachagua. Wao hawawezi kuendelea kuwa katika likizo wala kupewa nafasi tena isipokuwa tu uamuzi huo ubatilishwe