Habari

Afisa Mukhwana afikishwa mahakamani kuhusiana na kifo cha Ojwang

Na RICHARD MUNGUTI June 13th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

AFISA wa polisi James Mukhwana amefikishwa kortini kuhusiana na kifo cha mwalimu-bloga Albert Ojwang aliyekufa katika kituo cha polisi cha Central.
Hakimu mwandamizi Robinson Ondieki ameombwa na IPOA azuilie Mukhwana kwa siku 21 kuwezesha polisi kukamilisha  uchunguzi wa mauaji ya kinyama ya Ojwang.
Mkurugenzi wa Ipoa Mohammed Jibril ameomba afisa huyu wa polisi aliyekuwa na kifunguo cha seli katika kituo cha polisi cha Central azuiliwe kwa siku 21 ili asiwavuruge mashahidi.
Jibril aliambia mahakama mauaji ya Ojwang yalipangwa na kutekelezwa na maafisa wa polisi waliomkamata kutoka nyumbani kwake kaunti ya Homa Bay.
Hakimu alielezwa polisi wanatumia sheria zao za kudumisha usiri almaarufu Blue Code of Silence kuwaficha waliohusika na mipango na mauaji ya Ojwang.
Bw Ondieki alielezwa baadhi ya maafisa wa polisi waliohusika na mauaji ya kinyama ya Ojwang wamejificha.
Korti imeelezwa kuwa Rais William Ruto na bunge la Seneti na lile la Kitaifa yamejadili suala hili.
Hata hivyo mawakili Danstan Omari wameomba korti imwachilie Mukhwana kwa dhamana wakisema mshukiwa huyu alijisalamisha kwa IPOA.