Afisa wa kaunti aahidi uimarishaji zaidi wa miundomsing Nairobi
AFISA Mkuu wa Uchukuzi Kaunti ya Nairobi Michael Waikenda amesema kuwa utawala wa Gavana Johnson Sakaja utaendelea kuimarisha miundomsingi na kuhakikisha usalama wa wanaotumia njia zilizotengewa wanaotembea kwa miguu.
Bw Waikenda alisema kaunti imewekeza katika kuhakikisha ubora wa sehemu za barabara zinazotumiwa na wapitanjia, waendeshaji baiskeli na aina nyingine za uchukuzi.
Alisema miradi kama hiyo imetekelezwa maeneo ya Westlands, Ngara na katikati mwa jiji huku ikichangia kupungua kwa ajali na mizozo kati ya waendeshaji magari na wanaotembea kwa miguu.
“Nairobi imekuwa jiji la watu siyo magari pekee. Lengo letu ni kuhakikisha kuna mpangilio bora na uchukuzi unakuwa rahisi sana jijini,” akasema Bw Waikenda akikagua jinsi miundomsingi inavyoboreshwa jijini.
Alisema sehemu ya barabara inayotumiwa na wapitanjia kwenye barabara za Tom Mboya na karibu na Archives nazo zimechangia kupunguza msongamano wa magari.

Bw Waikenda pia aliongeza kuwa ni kutokana na miundomsingi bora ndio vijana wanaopiga picha sehemu mbalimbali wamepata ajira na wanajizimbulia riziki.
Maeneo ya Green Park na Desai nayo yameibuka kuwa vivutio kwa watengenezaji filamu na abiria kutokana na mandhari mazuri.
Afisa huyo alisema polisi wamekuwa wakitumia teknolojia ya Nairobi Dashboard kukagua na kudhibiti msongamano.
“Hii imesaidia kupunguza ajali za barabarani na kuimarisha ushirikiano kati ya polisi wa trafiki,” akasema.
Kaunti pia inapanga kushirikiana na sekta za kibinafsi kuimarisha uchukuzi wa mabasi ya umeme.
Bw Waikenda alisema kuwa lengo lao ni kubadilisha mienendo ambapo magari yalikuwa yakiegeshwa na kuendeshwa bila utaratibu kufuatwa katikati mwa jiji.