Afueni kwa wakazi benki ikifungua matawi matatu kwa mpigo
Benki ya I&M inaendelea kupanua mtandao wake wa matawi hata wakati huu ambao huduma za benki za kidijitali zinaendelea kubadilisha sekta ya kifedha.
Benki hiyo imefungua matawi matatu mapya katika Kaunti ya Kajiado—Ngong, Kitengela na Ong’ata Rongai—hatua iliyoongeza idadi ya kaunti zilizo na matawi ya I&M Bank hadi 28.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa tawi la Kitengela Jumanne, Mkuu wa Usambazaji wa I&M Bank, Stanley Gachoka, alisema ingawa wateja wengi wamekumbatia huduma za kidijitali, bado kuna huduma zinazohitaji kutangamana ili kuboresha uelewa na kujenga imani.
“Matawi yana jukumu muhimu katika kuimarisha ushirikiano na wateja, yakikamilisha majukwaa ya kidijitali badala ya kushindana nayo. Baadhi ya huduma hufanikiwa zaidi kupitia mawasiliano ya moja kwa moja na mteja,” alisema Gachoka.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Huduma za Rejareja wa I&M Bank, Shamia Patel, alisema huduma za benki za kidijitali na za kawaida huwa zinaenda sambamba huku benki ikilenga kupanua uwepo wake katika kaunti zote 47.
“Tunalenga ukuaji wa kidijitali na matawi kwa pamoja kama mkakati kamili unaoendana na mabadiliko ya sekta ya benki nchini. Tunakusudia kupanua matawi kote nchini na kutoa huduma bora kwa gharama nafuu ili kukuza mtaji wa wateja wetu,” alisema Patel.
Upanuzi huo unalenga miji inayokua kwa kasi, huku Kitengela ikitambuliwa kama soko lenye fursa kubwa ya ukuaji wa wateja.
I&M Bank imesema hatua hiyo ni sehemu ya mkakati mpana wa kuwafikia wateja huku ikiunga mkono ukuaji wa uchumi wa kidijitali nchini Kenya.