Ajabu Wakenya 40 walioenda kutafuta kazi Mynmar wakizuiliwa kama mateka
Waliondoka Kenya wakiwa na matumaini makubwa ya maisha bora.
Ahadi ya kazi ya uuzaji kidijitali nchini Myanmar kwa mshahara wa hadi Sh100,000 kwa mwezi iliwekwa mbele yao kama mwokozi katika taifa ambako ukosefu wa ajira unaendelea kuwanyima vijana fursa.
Lakini kwa sasa, ndoto hiyo imegeuka jinamizi kwa takriban Wakenya 40 wanaozuiliwa katika magereza ya Myanmar, maelfu ya kilomita kutoka nyumbani, baada ya kunaswa katika kile ambacho familia zao zinaamini ni ulaghai wa kimataifa uliojificha kama ajira ughaibuni.
Miongoni mwao ni John Kangi Kibe.
Alipoondoka Kenya Juni 2025 kuelekea Thailand, alimweleza rafiki yake Meshack Mutinda kuwa amepata kazi zuri ya uuzaji mtandaoni.
Hata hivyo, alipowasili Bangkok mambo yalibadilika.
Ofisi haikuwa Bangkok bali ilikuwa umbali wa saa mbili kutoka hapo, na kazi haikufanana na alichoahidiwa.
Baadaye alimweleza rafiki yake kuwa mahali hapo hapakuwa kama sehemu ya kazi bali kifungo, huku akifuatiliwa kila mara.
Siku moja kituo chao kilivamiwa na ndipo akajipata mikononi mwa watu asiyowajua.
Mwezi uliopita alimwambia rafiki yake kuwa angekuwa miongoni mwa Wakenya watakaorejeshwa nyumbani Januari 14, kwa sharti la kujilipia tiketi.
Hata hivyo, safari hiyo haikutimia. Mawasiliano yao ya mwisho yalieleza kuwa walipakiwa kwenye lori kuelekea mahali pasipojulikana. Tangu wakati huo, kimya kimetawala.
Abigael Cherop naye alinaswa katika mtego huo.
Kulingana na dadake Cynthia Jemutai, alielekezwa kwa “kazi ya uuzaji mtandaoni” Thailand. Lakini alipowasili, alifichua kuwa alikuwa akifanya kazi katika kampuni ya utapeli mtandaoni.
Baada ya miezi miwili, walivamiwa wakitarajia kurejeshwa nyumbani, lakini akajikuta tena katika mtandao mwingine wa ulaghai. Malipo yalitegemea kazi unayofanya, na mzunguko wa utapeli haukuisha.
Kwa Hosea Cheruiyot, aliondoka Desemba 21, 2025 akiaga mkewe Mercy Wafula na watoto wao watatu, wakitumaini maisha yangekuwa bora.
Walikuwa wameuza ng’ombe wao wa pekee kufadhili safari. Lakini baada ya kuwasili, alianza kulalamikia mazingira magumu ya kazi, na kucheleweshwa kwa mishahara. Mnamo Januari 7, 2026 alimwambia mkewe angefukuzwa nchini na kurejea nyumbani ndani ya wiki moja. Tangu hapo, hakusikika tena.
Victor Kipruto, mume wa Eunice Kavini, alitoa Sh150,000 kupata kazi Thailand.
Aliahidiwa kazi ya uuzaji lakini akajikuta katika mtandao wa utapeli. Mkewe anasema walipigwa wakishindwa kufikia malengo ya kila siku. Baadaye alisafirishwa hadi Myanmar na mawasiliano yalikatika.
Diana Gatwiri naye anamsubiri mumewe Fredrick Mwenda, aliyeondoka Agosti 2024 kwa kazi ya “mauzo ya kidijitali.” Iligeuka kuwa utapeli. Walionywa kuwa yeyote atakayejitahidi kutoroka angeuawa. Hadi sasa, anasubiri kwa hofu.
Alice Wanjiru aliandikia Wizara ya Masuala ya Kigeni kuhusu dadake Irene na Wakenya wengine 38. Aliarifiwa kuwa walikombolewa kutoka kituo cha utapeli na kuwekwa katika kambi ya kijeshi kabla ya kuhamishwa gereza la Hpa-An Januari 7. Tangu hapo, familia hazijapokea taarifa rasmi kuhusu hali zao.
Wizara ilijibu kuwa ilikutana na maafisa wa Myanmar Bangkok Januari 15, 2026 kuomba kuharakishwa kuachiliwa kwao, lakini ikaeleza haina mamlaka kuhusu taratibu za ndani za Myanmar.
Familia zilishangaa zilipoombwa kulipa Sh70,540 kwa tiketi za ndege kabla ya kuambiwa baadaye kuwa mahakama ya Myanmar imewahukumu kifungo cha mwaka mmoja kwa kuingia nchini humo kinyume cha sheria na kujihusisha na utapeli mtandaoni katika eneo la Bamboo Forest Site.
Mnamo Machi 5, 2025 Mbunge Mteule Irene Mayaka alihoji kuhusu usalama wa Wakenya waliokwama Myanmar. Alisema tangu 2022 mamia ya Wakenya wamenaswa na mtandao haramu wa ulanguzi wa watu unaojificha kama ajira Thailand. Wengi huahidiwa kazi na kuingizwa Myanmar.
Wakiwa huko, alisema, waathiriwa hulazimishwa kufanya kazi za utapeli mtandaoni na kukabiliwa na mazingira mabaya yasiyo na chakula, maji wala usafi.