Albert Ojwang’ hakujiua bali aliuawa kikatili, mpasuaji wa serikali atangaza
RIPOTI ya upasuaji uliofanyiwa maiti ya mwalimu, na mwanablogu, Albert Ojwang’ imebaini dalili kwamba alipigwa vibaya kabla ya kufa, huku mwanapatholojia wa serikali akisema hakujiua kwa kujigonga ukutani kama polisi walivyodai.
Akiongea baada ya kuendesha shughuli hiyo Jumanne Juni 10, 2025, katika hifadhi ya maiti ya City, Nairobi, Dkt Benard Midira alisema yeye na wanapatholojia waliowakilisha familia ya Ojwang na wadau wengine, walikubaliana kuwa kifo cha Ojwang kilisababishwa na watu wengine.
“Tulipata majeraha kwenye kichwa, dalili ya majeraha shingoni na sehemu zingine mwilini na miguuni,” akasema Dkt Midira.
“Majeraha hayo yanaonyesha kuwa alishambuliwa. Kulikuwa na dalili kwamba alipambana na washambuliaji wake akijaribu kujikinga,” akaongeza.
Dkt Midira aliongeza kuwa huku ikiwa vigumu kubaini wakati ambapo alipata majeraha hayo, yalitokea ndani ya muda mfupi.
“Alivuja damu kwenye ubongo…alitokwa na damu sehemu zingine za mwili. Hii inaonyesha kuwa hakujigonga,” akaongeza.
Rais wa Chama cha Wanasheria Nchini (LSK) Faith Odhiambo alielezea majeraha hayo kama yanayoonyesha kuwa Ojwang’ aliteswa kikatili, akisema wahusika walitekeleza mauaji ya kiholela.
“Kosa lake haitambuliwi kisheria. Kuna mtu aliyetoa amri Ojwang’ achukuliwe kutoka nyumbani kwao Homa Bay. Sharti mtu huyo awajibike,” akasema Bi Odhiambo.
“Tutaendelea kuweka presha hadi maafisa wote waliohusika wameadhibiwa kama watu binafsi. Sharti IPOA ichukue hatua, hatutakubali visingizio,” akaongeza.
Babake mwendazake Meshark Ojwang Opiyo, alielekeza lawama kwa mlalamishi Bw Eliud Lagat ambaye ni Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi (DIG)
“Ewe Eliud Lagat, je, ni wewe uliwatuma maafisa wako. Mbona uliua mtoto wangu. Alifanya kosa gani kupata adhabu kali kama hii? Mbona mtoto wangu alisalitiwa?” Mzee Opiyo akauliza.
– IMETAFSIRIWA NA CHARLES WASONGA