Ambia watu aliyeua Gen Z kwanza, Kalonzo ajibu Ruto kuhusu msamaha
VIONGOZI wa Upinzani wamekataa msamaha uliotolewa na Rais William Ruto wakati wa Maombi ya Kitaifa Jumatano.
Wakiongozwa na Kinara wa Wiper Kalonzo Musyoka ambaye alialika wenzake nyumbani kwake Tseikuru, Kaunti ya Kitui, viongozi hao walisema ombi la msamaha la Ruto lilinuiwa kufumba macho Wakenya baada ya kuhisi kwamba atashindwa kwenye Uchaguzi Mkuu wa 2027.
Bw Musyoka alisema ombi hilo lilikuwa kejeli kubwa kwa familia ambazo bado zinaomboleza watoto wao waliouliwa na risasi za polisi wakati wa Maandamano ya Kupinga Mswada wa Fedha 2024.
“Kwanza, ambia nchi nani aliua Gen Zs kabla ya kuomba radhi. Ukweli lazima ujulikane ili kutendeke haki kabla ya maridhiano,” akasema Kalonzo.
Kila aliyezungumza kutoka vyama kumi vilivyohudhuria hafla hiyo alisema hakuna msamaha bila kutubu na kwamba Rais lazima akiri madhila yaliyotendwa na serikali yake dhidi ya Wakenya.