Habari

Apatikana na vitambulisho 8 na pasipoti ya DRC Congo

Na RICHARD MUNGUTI March 6th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MSHUKIWA aliyekamatwa na polisi akiwa na vitambulisha vya kitaifa vinane vikiwa na picha yake na majina tofauti ameshtakiwa kwa ulaghai wa Sh52.5milioni.

Mbali na vitambulisho hivyo vinane Albert Komen Kipkechem almaarufu Jonathan Kiptum Barmasai alikutwa akiwa na pasipoti mbili-moja ya Kenya na nyingine ya nchi ya DR Congo.

Na wakati huo huo hakimu mwandamizi mahakama ya Milimani Nairobi alifahamishwa Albert Komen Kipkechem almaarufu Jonathan Kiptum Barmasai amehusishwa na ulaghai wa zaidi ya Sh100milioni.

Kipkechem ameshtakiwa kuvuruga mitandao ya mashirika yakifedha na benki kutekeleza uhalifu.

Alikana mashtaka mawili ya uhalifu wa kimitandao na pia kujipatia pesa kwa njia ya ulaghai Sh52,549,798 kutoka kwa kampuni ya Eclecities International.

Upande wa mashtaka ulipinga mshtakiwa huyo akiachiliwa jwa dhamana ukisema atatoroka punde atakapoachiliwa kwa dhamana.

“Kutokana na wingi wa vitambulisho alivyonavyo mshtakiwa na pasipoti mbili ni wazi kwamba akiachiliwa atatoroka kwa vile itakuwa vigumu polisi kumwandama,” hakimu alielezwa na kiongozi wa mashtaka Bi Joyce Olajo.

Wakili wa Bw Kipkechem aliomba mahakama azuiliwe katika kituo cha polisi cha Capitol Hill hadi Machi 12,2026 ndipo apate fursa ya kumhoji kuhusu madai ya upande wa mashtaka kuhusu vitambulisho, pasipoti na utapeli wa mamilioni ya pesa.

“Naomba Kipkechem azuiliwe hadi Machi 12 2026 nipate fursa ya kumhoji.Nilikabidhiwa afidaviti ya kupinga  mshtakiwa akiachiliwa kwa dhamana nikiwa hapa kortini.Nahitaji muda kuisoma na kupata maelezo kutoka kwa mshtakiwa,” wakili alimsihi hakimu.

Hakimu alikubalia ombi la wakili baada ya Bi Olajo kusema halipingi.