Babu Owino asema amepokonywa walinzi baada ya kushiriki maandamano
BUNGE wa Embakasi Mashariki, Babu Owino, amefichua kuwa serikali imeondoa walinzi wake rasmi, akidai hatua hiyo imetokana na kushiriki kwake katika maandamano yaliyofanyika Jumatano Juni 25.
Kupitia taarifa mbunge huyo alikashifu vikali serikali, akisema hatua hiyo ni shambulio dhidi ya demokrasia.
“Jana nilisimama na wananchi, si dhidi ya taifa. Nilitumia haki yangu ya kidemokrasia kuandamana kwa amani kupinga hatua za serikali inayowatelekeza raia wake,” alisema Owino.
“Leo, kama kisasi, serikali imeondoa walinzi wangu rasmi,” aliongeza.
Mbunge huyo ambaye alionekana miongoni mwa waandamanaji katikati ya Nairobi, alisema kuwa kuwanyanyasa viongozi waliosimama na wananchi ni ishara ya serikali inayokwepa kuwajibika kwa wananchi wake.
“Serikali inayowaogopa viongozi walio upande wa wananchi si serikali ya kuwahudumia raia, bali ya kukwepa uwajibikaji,” alisema Owino.
Akiwa kwenye maandamano hayo, Owino alishangiliwa na mamia ya vijana.
Maandamano hayo yaliandaliwa kukumbuka Gen Z waliopoteza maisha yao katika maandamano ya kupinga Mswada wa Fedha mwaka jana. Maandamano hayo ya siku nzima yaliambatana na makabiliano kati ya waandamanaji na polisi katika sehemu mbalimbali nchini, huku maafisa wa usalama wakijaribu kudhibiti hali.
Bw Owino alisisitiza kuwa ataendelea kusimama na wananchi, akisema ulinzi wake unatoka kwa Wakenya wenyewe. Aidha, aliwataka viongozi kutotishwa na serikali.
“Sihofii vitisho. Siwezi kunyamazishwa. Sauti yangu, na sauti ya kila Mkenya anayepigania haki, usawa na uhuru, itaendelea kuwa kubwa zaidi. Wakenya ndio walinzi wangu,” alisisitiza.
Owino pia aliwahimiza Wakenya kusimama kidete kutetea haki zao na kuwawajibisha viongozi wao, akisisitiza kwamba ataendelea kuunga mkono juhudi za kutafuta uongozi bora na wa kuwajibika.
“Kwa wananchi: endeleeni kuwa macho, muungane na mjue kuwa viongozi wenu wanapaswa kuwajibika kwenu – si kuwatisha wanaosimama pamoja nanyi. Ukweli hauwezi kufichwa. Harakati za kutaka haki hazitazimwa,” aliongeza.