Habari

Barabara kufungwa daraja likarabatiwe

Na ANTHONY KITIMO February 28th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MSONGAMANO wa magari unatarajiwa kushughudiwa leo mjini Mombasa baada ya barabara yenye shughuli nyingi kufungwa.
Shirika la Reli nchini limetangaza kusitishwa kwa muda kwa usafiri katika barabara ya Moi Avenue jijini Mombasa ili kuruhusu ukarabati wa daraja muhimu la reli eneo hilo.
Katika taarifa kwa umma iliyotolewa Ijumaa, shirika hilo lilisema sehemu ya barabara hiyo itafungwa Jumapili, Machi 1, 2026, kwa saa nne, kuanzia saa 12 asubuhi hadi saa 4 asubuhi.
“Shirika la Reli linapenda kuufahamisha umma kuhusu kusitishwa kwa muda kwa shughuli za usafiri katika Moi Avenue kufuatia kufungwa kwa sehemu ya barabara hiyo kama ilivyopangwa,” ilitangaza Shirika hilo.
Shirika hilo lilibainisha kuwa kufungwa kwa muda ni muhimu ili kuwezesha kazi za dharura za ukarabati zilizopangwa kwenye daraja la Reli la Mbaraki linalopita juu ya barabara lililopo kando ya Moi Avenue.
KRC pia ilisisitiza kuwa kazi hizo zilizopangwa ni muhimu ili kuhakikisha usalama na uthabiti wa miundombinu ya reli na kuepusha ajali au matukio yoyote yajayo.
Madereva wanaotumia barabara hiyo yenye shughuli nyingi wameshauriwa kupanga safari zao mapema na kutumia barabara mbadala zilizoainishwa wakati wa kufungwa kwa saa nne.